Nigeria: Watiwa mbaroni kwa tuhuma za kula mchana wakati wa Ramadhani, wenyewe wadai binafsi hawakuuona mwezi
Polisi wa Sharia ya Kiislamu katika jimbo la kaskazini mwa Nigeria la The Islamic Sharia Kano wamewakamata kwa muda watu 80 walioshutumiwa kwa kula hadharani kipindi cha mchana, badala ya kufunga kuanzia alfajiri hadi jua linapotua kulingana na maagizo ya dini ya kiislamu katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.
Polisi wa Sharia , wanaofahamika kama Hisbah, wanasema kuwa watu hao walikamatwa kwa nyakati tofauti katika maeneo mbali mbali ya mji wa Kano kipindi cha siku kadhaa.
Jimbo la Kano ni moja kati ya majimbo kadhaa ya kaskazini mwa Nigeria ambako Sharia ya kislamu ilianzishwa upya tangu mwaka 2000. Sharia ya kiislamu inatekelezwa sambamba na sheria ya kawaida kwenye majimbo hayo.
Msemaji wa Hisbah katika jimbo la Kano, Adamu Yahaya, ameiambia BBC kuwa wote waliokamatwa walikuwa ni Waislamu na maafisa hawawalengi wasio Waislamu kwasababu hawafungwi na sheria ya kiislamu.
Amesema kuwa baadhi ya wale waliokamatwa waliiambia ofisi ya Sharia kuwa walikuwa wanakula kwasababu hawakuuona binafsi mwezi wa Ramadhani huku wengine wakisema walikuwa ni wagonjwa, lakini maafisa walisema kuwa madai yao hayakuwa na msingi wowote.
Watu hao 80 walionywa na kuachiliwa huru kwasababu walikuwa wamefanya kosa hilo kwa ”mara ya kwanza” alisema Bwana Yahaya.
Walionywa kuwa iwapo watakamatwa tena, watapelekwa mahakamani.
Hisbah wamesema kuwa wataendelea kufanya doria katika kipindi chote cha ramadhani kwa lengo la kuwakamata waislamu wote ambao hawafungi katika mwezi huu.
Mfungo wa Ramadani ni lazima kwa kila mtu mzima muislamu , lakini baadhi ya watu kama vile wenye magonjwa makubwa – hawatakiwi kufunga.
- Ramadhan ni moja ya nguzo tano kuu katika dini ya Kiislamu.
- Mwezi huo, Waislamu hujifunga kula na kunywa kuanzia macheo hadi machweo.
- Kufunga wakati huu huwawezesha Waislamu kujitolea zaidi katika dini na kumkaribia Allah.
- Kando na kufunga, ni wakati pia wa kutafakari kiroho, kuswali, kutenda matendo mema na kujumuika na familia na marafiki.
Waislamu hufanya juhudi za kipekee kuungana na wengine katika jamii na kuwasaidia wale wanaohitaji usaidizi katika jamii.
Huwa ni kawaida kwa Waislamu kula chakula asubuhi kabla ya mawio, suhur, na jioni wakati wa kufungua baada ya jua kutua, ambacho hufahamika kama iftar.
Mwisho wa kufunga, baada ya machweo, familia na marafiki hujumuika pamoja kufungua.
Wengi pia huenda Msikitini kuswali.
Ramadhan imekuwa mwezi huu kwa sababu ndio wakati Koran tukufu ilipofichuliwa kwa mara ya kwanza kwa Mtume Muhammad.
Ramadhan huwa ni mwezi wa tisa katika kalenda ya Kiislamu, lakini tarehe hiyo hubadilika kila mwaka.
Hii ni kwa sababu dini ya Kiislamu hufuata kalenda inayotumia mzunguko wa mwezi, hivyo hubadilika tofauti na kalenda inayotumiwa na mataifa ya Magharibi inayofuata jua.