UGANDA: Kisa cha kwanza cha ugonjwa wa Ebola charipotiwa, shirika la afya duniani (WHO) lathibitisha
Mtoto wa miaka mitano nchini Uganda apatikana kuwa na Ebola, shirika la afya duniani (WHO) limethibitisha. Hiki ni kisa cha kwanza kuthibitishwa katika nchi hiyo wakati kukishuhudiwa mlipuko wa ugonjwa huo katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidmeokrasi ya Congo.
Kwa mujibu wa shirika la habari la BBC, Zaidi ya visa 2,000 vimenakiliwa huko katika muda wa miezi 10 iliyopita – wengi wa waathirika wakifariki. Inaarifiwa kuwa mtoto huyo wa kivulana alisafiri na familia yake na kuvuka mpaka kutoka Congo siku ya Jumapili.
Baada ya hapo alipelekwa katika hospitali moja nchini Uganda baada ya kuonyesha dalili ikiwemo kutapika damu, maafisa wamesema.
Uthibitisho kwamba ni ugonjwa wa Ebola ulitolewa na taasisi ya kupambana na virusi nchini Uganda Virus Institute (UVRI) jana Jumanne kal aya kutangazwa rasmi na maafisa jana usiku.
Wizara ya afya nchini na WHO wanasema wametuma kikosi maalum kutambua wengine walio katika hatari, taarifa ya pamoja imeeleza.
Waziri wa afya Uganda Jane Ruth Aceng amewaambia wanaandishi habari kwamba familia ya mtoto huyo wanaangaliwa, wakiwemo wawili walionyesha kuwa na dalili za kama za ugonjwa wa Ebola.
Baada ya hapo alituma ujumbe kwenye Twitter akieleza kwamba nchi hiyo imeingia katika ‘hali ya muitikio’kufuatia kisa hicho.
Uganda has been in preparedness mode ever since the #Ebola outbreak was declared in DRC.
Now, we move into response mode.
Please cooperate with our health,immigration and security officials to ensure effective screening to prevent spread of #Ebola to other parts of the country.— Dr. Jane Ruth Aceng Ocero (@JaneRuth_Aceng) June 11, 2019
Tayari wahudumu 4, 700 nchini Uganda wamepewa chanjo dhidi ya ugonjwa huo, taarifa hiyo ya pamoja ya shirika la afya duniani na wizara ya afya nchini imeendelea kueleza.
Mlipuko huo katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo ni wa pili kwa ukubwa katika historia, huku kukishuhudiwa ongezeko la visa vipya katika wiki za hivi karibuni.
Takriban watu 1,400 wamefariki kutokana na ugonjwa huo tangu Agosti.
Ni mara moja tu ambapo ugonjwa huo umewahi kuendelea kuwa na makali zaidi ya miezi minane baada ya kuanza – na lilikuwa janga lililoshuhudiwa Afrika magharibi kati ya mwaka 2013 na 2016 lililosababisha vifo vya watu 11, 310.
Ebola ni nini?
- Ni ugonjwa unao sambaa haraka na hupelekea vifo vya asilimia 50 ya waathirika
- Dalili za awali ni homa ya ghafla, uchovu kupita kiasi, maumivu ya mishipa na koo.
- Dalili za hatari ni kutapika, kuharisha, na kwa kesi zingine ni kutoka damu ndani na nje ya mwili.
- Ebola huwapata binadamu wanapo gusana na wanyama walio athirika wakiwemo sokwe mtu, popo na paa.
- Watu wanaambukiza endapo damu zao na maye vimebeba vijidudu, na hii inaweza fika mpaka wiki saba tangu mtu alipopona.