Mo Salah asisitiza kiatu cha dhahabu ndiyo lengo lake kuu EPL
Mshambuliaji wa klabu ya Liverpool, Mohamed Salah amesisitiza kuwa lengo lake kuu msimu huu ni kutwaa tuzo ya mfungaji bora huku akiamini kuwa bado anavitu vingi vya kuonyesha Ligi kuu ya Uingereza na wala hafanyi yote kwa sababu ya kupata nafasi kujiunga ndani ya kikosi cha Chelsea kama inavyoelezwa.
Salah ambaye anajumla ya mabao 30 kwenye ligi kuu ya Uingereza msimu huu akimzidi mchezaji wa timu ya Tottenham, Harry Kane zaidi ya manne huku ikiwa imesalia michezo minne pekee kabla ya kumalizika kwa ligi hiyo.
Kupitia mahojiano na Sky Sports mara baada ya mchezo wao na West Brom, Salah amesema “Unaweza kuona michezo kadhaa iliyopita, wachezaji wanajaribu kunisaidia sana kufunga magoli, kwasababu wanafahamu kuwa nipo katika mbio za kuwania kiatu cha dhahabu lakini mwisho wa siku ni zawadi ya mtu binafsi lakini pia kufanya hivyo huisaidia timu,”amesema Salah.
Mo Salah ameongeza “Kwa namna tunavyocheza hakika inavutia na unaweza kuona mashabiki wakiwa na furaha kiasi ambacho najisikia vizuri kwa hilo nadhani wanahitaji kuniona nikishinda kitu fulani. ”
Takwimu zikionyesha kuwa kwenye kila mchezo ana goli moja la ugenini ligi ya Uingereza rekodi ambayo iliwahi kuwekwa na wachezaji kama, Alan Shearer msimu wa mwaka (95/96), Cristiano Ronaldo mwaka (07/08) na Luis Suarez mwaka (13/14), hata hivyo inaelezwa kuwa Salah husema kuwa timu ni lazima kupata matokeo kwanza licha ya kuwa na hamu ya kuitawala nafasi ya kwanza ya ufungaji.