Bolivia inaingia kwenye mzozo mpya baada ya seneta wa upinzani Jeanine Anez kujitangaza rais wa mpito wa taifa hilo linalokabiliwa na sintofahamu ya kisiasa muda mfupi tu baada ya aliyekuwa rais nchi hiyo, Evo Morales kujiuzulu na kukimbilia uhamishoni Mexico.
Bunge liliitishwa ili kuhalalisha hatua hiyo ya kujiuzulu na kumthibitisha naibu spika huyo wa Seneti kuwa rais wa mpito. Ingawa kikao hicho kilishindwa kufikisha idadi ya wabunge ili kuthibitisha uteuzi wake, lakini Anez alijitangaza kuwa rais wa mpito.
Mahakama ya katiba baadae ilimuidhinisha Anez. Hatua hiyo inaibua wasiwasi wa machafuko zaidi kufuatia wiki kadhaa za maandamano ya kupinga uchaguzi wa urais wa Oktoba 20.