Habari

Ashikiliwa na Polisi kwa tuhuma za kutupa mtoto chooni

Mwanamke aliyejulikana kwa jina la Neema Japhet (23) anashikiliwa na Polisi kwa tuhuma ya kumtupa mtoto wa siku moja kwenye choo cha Africa Inland Church Tanzania (AICT) mtaa wa Kitangiri, Manispaa ya Shinyanga baada ya kujifungua.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani humo, Elias Mwita aliwaeleza waandishi wa habari kuwa asubuhi jana mwanamke huyo alikamatwa na majirani zake chumbani kwake alikopanga eneo la Kitangiri na kisha kutoa taarifa polisi.

Mwita alisema mwanamke huyo alikamatwa na Polisi kwa tuhuma ya kumtupa mtoto wa siku moja chooni baada ya kujifungua Ijumaa wiki iliyopita, na kwa mujibu wa maelezo yake baada ya kuhojiwa alikiri kufanya kitendo hicho.

“Baada ya tukio hilo na mtu kutojulikana aliyefanya kitendo hicho, tulitoa wito kwa wananchi ili kuweza kumbaini, lakini juhudi za wananchi za kumsaka zimezaa matunda sasa majirani wameweza kumbaini mwanamke huyo ndiye aliyehusika na unyama huo,amekiri kuhusika na utupaji wa mtoto,” alieleza Kamanda Mwita.

Aidha Kamanda Mwita alisema saa tisa ya Januari 21, mwaka huu mwanamke huyo alionekana kwenye eneo la kanisa hilo, na baada ya kumhoji kwa mujibu wa maelezo yake, alieleza kuwa alikwenda chooni kwa lengo la kujisaidia, lakini ikatokea bahati mbaya mtoto kutumbukia kwenye tundu la choo.

BY: Emmy Mwaipopo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents