Bastian Schweinsteiger atangaza kustaafu soka la kimataifa
Mchezaji na kiungo wa Manchester United, Bastian Schweinsteiger, ametangaza kustaafu kuitumikia timu ya taifa ya Ujerumani, ikiwa ni majuma kadhaa baada ya timu hiyo kushindwa kufikia malengo ya kutwaa ubingwa wa barani Ulaya.
Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 31, alikuwa sehemu ya mafanikio yaliyopatikana wakati wa fainali za kombe la dunia za mwaka 2014, ambapo Ujerumani walitwaa ubingwa wa fainali hizo katika ardhi ya Brazil kwa kuifunga bao moja timu ya taifa ya Argentina.
Schweinsteiger, ametangaza kustaafu soka la kimataifa huku akiacha kumbu kumbu ya kuitumikia timu ya taifa ya Ujerumani katika michezo 120 sambamba na kufunga mabao 24.
“Katika michezo 120 niliyocheza nikiwa na timu yangu ya taifa, sina budi kujivunia kwa mafanikio niliyoyapata na ninaamini kipindi hiki ni sahihi kwangu kutangaza kuachana na timu hiyo, ili kupisha wachezaji wengine,”Imeeleza taarifa ya Schweinsteiger.