Burudani

Busara inahitajika kutafsiri tweet ya Davido baada ya ushindi wa Idris kwenye Big Brother

Katika siku ambayo Davido aliwakera watumiaji wa mitandao ya kijamii nchini Tanzania ni Jumapili hii. Baada tu ya Idris Sultan kutangazwa mshindi wa Big Brother Africa, Davido alitweet kitu ambacho hakujua kingewakera Watanzania wengi walioiona. “N they cheat again lol,” aliandika Davido kwa kuongeza na ‘Emoji’ ya kipaka kilichofunika macho yake.

Diamond na Davido wakicheza kwa madaha

Dakika chache tu baada ya muimbaji huyo wa Nigeria kuandika hivyo, mastaa mbalimbali wa Tanzania na watumiaji wengine wa Twitter walianza kumshambulia kwa matusi staa huyo. Wengi waliscreeshot tweet hiyo na kuipost kwenye Instagram na kumchana vikali. Wapo walimuita shoga, wengine wamemuita snitch, wengine wanamuita hater na wengine wamefikia hatua ya kumwambia mpenzi wake anacheat na Mtanzania!

Tweet hiyo imewakasirisha wabongo kiasi ambacho Nay wa Mitego ameahidi kumtwanga DJ yeyote atakayemsikia akicheza wimbo wake.

Lakini tumejaribu kuitafsiri maana halisi ya alichokiandika staa huyo au tunakuza mambo kutokana na hasira ya kuwa na maana yenye upande mmoja? Kunaweza kukawa na tafsiri nyingi ya hicho alichokiandika. Kwakuwa hajapenda kufafanua, bado alichomaanisha anakijua yeye mwenyewe na Mungu. Lakini tafsiri maarufu iliyowafanya watanzania wengi wamtukane, ni kuwa Tanzania imedanganya kupata ushindi wa Big Brother.

Hebu tuangalie mantiki ya tafsiri hii. Big Brother ni shindano linaloandaliwa na Multi Choice na Endemol, hushirikisha kampuni maalum ambalo husimamia shughuli za upigaji kura na kuwapa matokeo waandaji hao. Hakuna uwezekano wowote Tanzania imeweza kudanganya hadi kumfanya Idris awe mshindi.

Na pia, hata kama Tanzania nzima ingempigia kura Idris (kitu ambacho hakiwezekani sababu BBA ni shindano linaloangaliwa zaidi na watu wenye DSTV nyumbani kwao ambao hatudhani kama wanafikia asilimia 5 nchi nzima, ama wale ambao ni watumiaji wa mitandao ya kijamii kujua kinachoendelea hata kama wasipoangalia TV), kwa mfumo wa shindano hilo, Tanzania ina kura moja tu.

Hivyo ushindi wa Idris umepatikana kwa mkusanyiko wa kura moja moja za nchi mbalimbali barani Afrika, kumzidi Tayo wa Nigeria.

Tunaamini hili Davido analifahamu pia, hivyo tweet yake ilikuwa ikiwaendea moja kwa moja waandaaji wa shindano hilo na sio Watanzania kama wengi walivyoitafsiri. Na katika mashindano kama haya, tweet kama ya Davido ni za kawaida kwakuwa zimekaa kishabiki zaidi.

Kama walivyopenda wanaijeria wengine, Davido pia alitamani Tayo ashinde na kwa kwakuwa walikuwa na matarajio hayo bila kugundua nguvu ya Idris kwenye shindano hilo, kilikuwa ni kitu cha kawaida kuandika hivyo. Davido na wanaijeria wengine, wameshindwa kujua kuwa Idris alikuwa na kula za uhakika kutoka Tanzania, Uganda, Kenya, Namibia, Botswana Afrika Kusini na kwingine. Hawakutaka kukubali kuwa Idris alikuwa na nguvu zaidi kumzidi Tayo.

Wanaijeria wameumizwa kwakuwa mara yao ya mwisho kuchukua taji hilo ni mwaka 2011 kwenye msimu wa sita ambapo Karen Igho alishinda. Waliichukulia Hotshots kama nafasi pekee ya kurudisha heshima ya nchi yao wanayoamini kuwa ina nguvu kuliko mataifa mengine ya Afrika.

Aliposema ‘they cheat again’ ni wazi alimaanisha Biggie amelitoa taji hilo kwa nchi nyingine zaidi ya Nigeria kwa mwaka mwingine, baada ya mwaka jana kwenye Namibia kwa Dillish na mwaka 2012 kwenda kwa Keagan Petersen wa Afrika Kusini. Hajasema Tanzania imedanganya! Kwahiyo Davido anaonewa kwa kubebeshwa mzigo kutokana na tweet yake ya kishabiki.

Tweet ya Davido haina uhusiano wowote na ushindi wa Diamond kwenye tuzo za Channel O

Tafsiri nyingine ya tweet ya Davido ni kuwa Tanzania imedanganya tena baada ya Diamond hivi karibuni kushinda tuzo mbili za Channel O. Hii ni tafsiri isiyo sahihi kabisa na hapa Watanzania tunamuonea Davido waziwazi. Hivi mnasahau kuwa ni Davido ndiye alimpongeza kwa moyo mweupe kabisa Diamond kwenye Instagram? “TANZANIA STAND UP! HE DID IT! @diamondplatnumz.” Tumesahau mapema hivi wakati ni sisi wenyewe ndio tuliompongeza kwa ujasiri wake huo? Leo hii tunarudi kwenye post hiyo hiyo na kuanza kumtukana?

Kuna wasanii wengi tu maarufu hapa Tanzania hadi leo wameshindwa kumpongeza Diamond kutokana na chuki zao binafsi lakini Davido aliyekuwa akishindana naye kwenye kipengele kimoja alimpongeza Diamond. Na pamoja na kukosa tuzo zote tano, alikuwa na kifua kipana cha kuweza hata kuandika:
“Always will be grateful!!! More to come.”

Kwanini tunataka kujiaminisha kuwa anamchukia Diamond? Amchukue kwa lipi wakati Davido alikuwa ametajwa kuwania tuzo tano na ni moja tu ndiyo walikuwa wametajwa kuwania pamoja na Diamond? Pamoja na jitihada zake binafsi, tunasahau kuwa Davido ana mchango wake muhimu kwa mafanikio aliyonayo sasa Diamond? Kwanini hatuna shukrani na tayari tunaanza kutukana wakunga? Leo hii mtu huyu anageuka adui yetu kwa tweet ambayo tumeielewa vibaya?

Kosa lake pengine ni kuendelea kuwa na ego na kutotaka kutoa ufafanuzi wa kile alichomaanisha lakini matusi haya tunayoyaelekeza kwake yana hasara nyingi kuliko faida.

Kama tukifuata kauli ya Nay wa Mitego kuwa redio zisipige nyimbo zake, hiyo si njia ya kupunguza ukoloni wa Naija uliotawala vituo vyetu vya redio sababu hakuuanzisha yeye. Bado redio zitaendelea kupiga nyimbo za akina P-Square na wengine ambao hata kesho wakija Leaders, lazima pajae.

Na je tunavyoendelea kutengeneza uadui huu wa Nigeria na Tanzania, vipi na wao wakiamua hizo nyimbo za wasanii wawili watatu wanazopiga kwao wazichinjie baharini, hasara itarudi kwa nani?
Kinachosikitisha zaidi ni Diamond kuwa mmoja wa watu walioitafsiri tweet yake vibaya. Labda kama kuna vitu vingine vya chini chini vinavyoendelea kati yao ambavyo sisi hatuvijui, lakini tayari uhusiano wa wawili hao unaweza ukawa umeshaingia dosari.

“Thanks God, we have cheated another one on The Future Awards Africa in Lagos Nigeria… #SameDay #SameNight Thank you Allah!,” ameandika Diamond baada ya kushinda tuzo za TFA zilizotolewa jana huko Lagos.

Tunahitaji busara sana kujibu kauli za aina hii. Tunaweza tukaanza kubomoa tunachokijenga bila kujua.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents