Chris Brown apata msala mwingine, ni wa kumpiga mtu!
Chris Brown ameunusa tena mtungi wa sheria. Staa huyo wa R&B anachunguzwa kufuatia tukio la kupigwa mtu lililotokea Jumatatu hii kwenye hoteli ya Palms Casino Resort, Las Vegas.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na polisi wa Las Vegas, polisi walipokea simu kutoka hospitali ya Sunrise ambapo mwanaume mmoja alikuwa akitibiwa kwa majeraha ya kawaida kutokana na kupigwa.
Brown alikuwa akicheza kikapu kwenye hoteli hiyo na kuanza kurushiana maneno na mtu waliyekuwa wakicheza naye na kuzuka ugomvi wa ngumi. Mtu huyo amedai kuwa alipigwa ngumi na Brown na wakati anajitetea alipigwa na mtu mwingine anayedaiwa kuwa upande wa Brown.
Kwa mujibu wa mtandao wa ThisIs50, Brown alikuwa akicheza kikapu na muimbaji mwenzie Jeremih ambapo baada ya timu ya Jeremih kushinda kukafanyika mechi ya marudiano na ndipo ugomvi ulipozuka.
Polisi walishindwa kuzungumza na Brown walipowasili kwenye hoteli hiyo.