First Look: Cover ya filamu ya ‘Karibu Kiumeni’ imetoka
Katika filamu zilizofanyika Tanzania zinazosubiriwa kwa hamu zaidi, Karibu Kiumeni inashika nafasi ya kwanza. Ni kwasababu inatabiriwa kuja kuwa filamu ya Kitanzania itakayopata mafanikio makubwa kutokana na kutengenezwa kwa ueledi wa hali ya juu.
Na sasa cover la filamu hiyo limeoneshwa kwa mara ya kwanza. Karibu Kiumeni imeigizwa na Ernest Napoleon (maarufu kwenye filamu ya Going Bongo), Irene Paul, Idris Sultan, Antu na waigizaji wengine.
Filamu hiyo pia itakuwa na soundtrack itakayokutanisha mastaa kibao wa Bongo Flava na kusimamiwa na mtayarishaji mkongwe, P-Funk.
“Ngoma zitakuwa kama sita, moja itakuwa Nature na Inspekta, watafanya ngoma itakayobeba jina la movie na maudhui ya Temeke,” Napoleon aliiambia Bongo5. “Itakuwa ngoma ya kwanza ya kurap pamoja tokea Mzee wa Busara,” aliongeza.
Pia anasema kwenye soundtrack hiyo, TID atafanya ngoma na Adili huku Fid Q akifanya na AY.
“Damian Soul pia atafanya Ngoma ya mapenzi, halafu Msaga Sumu Singeli. Wengine watakuwepo kama Young Killer, Dogo Janja, watafanya ngoma ya pamoja ya generation yao.”
Karibu Kiumeni inatarajiwa kuzinduliwa mwishoni mwa mwaka huu.