Kocha wa Aston Villa aondoka baada ya siku 147
Uongozi wa klabu ya Aston Villa, umemalizana na kocha huyo raia wa Ufaransa, Remi Garde ameondoka katika kilabu hiyo kupitia maelewano baada ya kuhudumu kwa siku 147 katika kilabu hiyo iliopo katika mkia wa jedwali la ligi ya Uingereza.
Mwenyekiti mpya wa klabu ya Aston Villa, Steve Hollis pamoja na mkurugenzi David Bernstein walifikia maamuzi ya kumtimua kazi meneja huyo na kutoa taarifa wakati mchezo wa kimataifa wa kirafiki kati ya England na Uholanzi ukiendelea usiku wa kuamkia hii leo.
Baadhi ya mameneja kama Nigel Pearson, Sean Dyche pamoja na Steve Bruce wanatajwa huenda mmoja wao akapewa jukumu la kuinusuru Aston Villa isishuke daraja msimu huu.
Katika utawala wa Garde, Aston Villa imefanikiwa kushinda michezo miwili kati ya ishirini iliyochezwa akiwa kama mkuu wa benchi la ufundi, hali ambayo imepelekea klabu hiyo ya Villa Park kuendelea kuburuza mkia wa msimamo wa ligi ya nchini England.