Habari

Serikali yahamasisha kilimo cha mazao makuu matano

Serikali inaendelea na mpango wa kuhamasisha ulimaji wa mazao makuu matano ya Pamba, Korosho, Tumbaku, Kahawa na Chai nchini ili kuongeza uzalishaji wa mazao hayo.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameyasema hayo Bungeni Mjini Dodoma wakati wa maswali kwa Waziri Mkuu alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Sumve Mhe. Richard Ndassa juu ya namna Serikali ilivyojipanga na utafutaji wa masoko ya Pamba kutokana na mwitikio mkubwa wa kulima zao hilo mwaka huu.

“Miongoni mwa mikakati ya kuendeleza mazao hayo ni pamoja na kulima kisasa na kutafuta masoko ndani na nje ya nchi,” alisema Waziri Mkuu.

Amesema, mwezi huu anatarajia kukutana na watumiaji wa zao la Pamba hapa nchini ili kuweka mfumo endelevu wa ununuzi wa zao hilo. Aidha, Wizara ya Kilimo inafanya kazi ya kutafuta masoko nje ya nchi.

Pia, Mhe. Majaliwa alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Liwale Mhe. Zuberi Kuchauka juu ugawaji wa pembejeo za korosho kwa mwaka huu amesema, Serikali ilitoa pembejeo ya Salfa bure mwaka jana kwa wakulima wa korosho ili kufanya hamasa kwa zao hilo baada ya wakulima kutelekeza zao hilo kutokana na kukosa pembejeo hiyo.

“Baada ya ugawaji wa pembejeo hiyo ya Salfa zao hilo limevunwa kwa kiwango cha juu kwa mwaka jana, hivyo kutokana na fedha walizozipata wakulima wa zao hilo watatatikiwa kuchangia gharama za Salfa kwa mwaka huu,” alisema Mhe. Majaliwa.

Wakati huo huo, Mhe. Kassim Majaliwa alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Urambo Mhe. Margaret Sitta juu ya migogoro ya mipaka ya mapori na misitu, amesema Serikali imeiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kushirikisha wanavijiji na viongozi wa kijiji wakati wa uwekaji wa mipaka hiyo.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents