Habari

Zilizotufikia: Roma na wenzake wapatikana wakiwa salama

Taarifa zilizotufikia zimedai kuwa Roma na watu wengine waliokuwa wameshikiliwa tangu Jumatano hii wamepatikana wakiwa salama.

Mkuu wa polisi (OCD) wilaya ya Kinondoni, Abubakar Kunga amethibitisha kupatikana kwa wote waliopotea. Lakini kwa sasa amesema wanafanya nao mahojiano ya kipolisi katika kituo cha Oysterbay lakini baada ya muda mfupi wataongea na waandishi ili kutoa taarifa kamili.

Kupatikana kwao kumefuatia wito mkubwa uliokuwa ukipaishwa na wasanii wenzake na mashabiki kuhusu kuachiliwa huru.

Awali, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, Kamishina Simon Sirro alisema bado walikuwa wakiendelea na upelelezi wa tukio la kupotea (kutekwa) kwa msanii Roma Mkatoliki na wenzake.

Akiongea na waandishi wa habari mchana huu Polisi Central jijini Dar es salaam, Kamanda Sirro alisema tukio la utekwaji wa Roma na wenzake ni aina ya matukio ambayo hutokea mara kwa mara.

“Matukio ya utekaji hayajaanza leo, hili la kina Roma na wenzake ni tukio kama matukio mengine yaliyokuwa ya ujambazi kwahiyo tupeni muda tupeleleze, tukifika mahali pazuri tutawaita tuwape taarifa lakini nimeona mitandao mingi inazungumza, jana nikaona wasanii wamekutana lakini nikajiuliza hivi yangekuwa haya matukio yanatokea ya uhalifu yanapotokea watu wanakutana ingekuwaje?,” alisema Sirro.

Aliongeza, “Jamani kazi hii tumepewa kwa mujibu wa Katiba na ni lazima tutimize wajibu wetu kwa hiyo tupeni muda tutakuwa na majibu mazuri katika hili,” aliongeza.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents