Tetesi: Huduma ya Taxi za Uber kuingia Dar es Salaam ‘soon’
Baada ya Uber kuanza kufanya kazi jijini Nairobi, Kenya, kuna tetesi kuwa huduma ya taxi hizo zisizo rasmi iliyopo kwenye majiji 375 duniani itaingia Dar es Salaam hivi karibuni.
Uber ni nini?
Ni huduma ya taxi (usafiri) kutumia application ya simu iitwayo Uber. Ipo kwenye simu za iPhone au Android.
Inafanyaje kazi?
Kwanza Uber, iliyoanzishwa na kampuni ya Uber Technologies Inc. ya San Francisco, California nchini Marekani, hutumia madereva wenye magari wanayoyamiliki wao wenyewe. Uber haina gari hata moja, bali huwatumia watu binafsi wenye magari yao waliojiandikisha kutoa huduma hiyo. Hadi mwishoni mwa mwaka jana, Uber ilikuwa na thamani ya dola bilioni 62.5.
App yenye inafanya kazi vipi?
Ukishadownload app ya Uber, ifungue na kufungua akaunti yako. App hiyo itapata eneo ulilopo kwa kutumia GPS na kukuonesha ramani. Unachotakiwa kufanya ni kuonesha tu wapi unapotaka kuja kuchukuliwa na taxi kwa kusogeza kile kialama chekundu hadi pale ulipo na kisha unabonyeza kitufe cha kijani cha “set pickup location” kisha kile kitufe kilichoandikwa “request pickup here.”
Ukimaliza, dereva atakubali ombi lako na kisha utapokea ujumbe utakaokueleza jina la dereva na atawasili muda gani kukuchukua.
Utapata ujumbe mwingine kuwa dereva amefika. Ingia kwenye gari, mwambie dereva unapoenda na unapofika shuka kwenye gari nenda zako. Huhitaji kumlipa hela sababu hela ya nauli itakatwa moja kwa moja kwenye credit card yako uliyoiandikisha wakati unafungua akaunti yako.
Huduma hii itatengeneza ajira kwa watu wengi wenye magari madogo na hata ambao kwa sasa hawafanyi kazi kama madereva taxi.