Wachezaji watano na makocha wawili Barcelona wakutwa na Virusi vya Corona, ukweli wafichwa
Wachezaji watano wa kikosi cha kwanza cha Barcelona na kocha wawili wamekutwa na virusi vya Corona baada ya kufanyiwa vipimo lakini inadaiwa kuwa miamba hiyo ya soka ya LaLiga iliamua kufanya siri.
Kwa mujibu wa Radio ya RAC1, kutoka Katalunya imeripoti habari hiyo katika kipindi cha cha ‘Tu Diras’ wakati huu ambao Barca na baadhi ya klabu nyingine za LaLiga zinajiandaa kurejea tena kwa msimu wa soka Juni 11 mwaka huu wa 2020.
Nyota hao watano ambao majina yao hayakutajwa, wanadaiwa hawakuwa na dalili zozote za ugonjwa huo na mara baada ya vipimo ndipo wakabaini kuwa na virusi vya Corona.
Hata hivyo wachezaji hao watano ambao walikutwa na Corona tayari wameshapona na wenye afya njema na sasa wanatarajiwa kurejea tena kwenye mazoezi.
Inadaiwa mabingwa hao wa soka Hispania walishindwa kuweka wazi taarifa hiyo kwa jamii na sasa wanatoa maoni yao juu ya ripoti iliyotolewa na RAC1.
Taarifa hiyo iliyoripotiwa na RAC1 haijathibitishwa na klabu yenyewe wala katika ripoti za kesi za virusi vya corona kutoka chama cha soka LaLiga.
Barcelona inatarajiwa kurejea tena uwanjani wakiwa ugenini dhidi ya Mallorca, Juni 13 baada ya LaLiga kuonyesha ishara ya kurejea tena mwezi huu.