Habari

CCM yafuta uchaguzi kata 41

Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeanza kupeleka salamu kwa wagombea wa nafasi mbalimbali, wanaokiuka Katiba na Kanuni za Uchaguzi, baada ya kufuta uchaguzi wa ndani ya chama hicho katika kata 41 kati ya kata 4,420 zinazoshiriki katika uchaguzi huo, kutokana na kubaini mchezo mchafu na kuagiza mchakato kurejewa upya.

Hayo yalibainishwa jana Dar es Salaam na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) wa Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole alipozungumza na waandishi wa habari.

“Hii ni awamu ya kwanza tunapeleka ujumbe kwa sababu wanaCCM wanataka CCM mpya inayosimamia haki, haya ni maelekezo na yanapaswa kuzingatiwa ili kurejesha hali ya uchaguzi katika eneo husika katika namna inayoheshimu Katiba na Kanuni ya Uchaguzi na Uongozi na Maadili,” alifafanua Polepole.

Polepole alibainisha kuwa kufutwa kwa uchaguzi huo ni agizo la viongozi wa juu wa chama hicho akiwemo Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais John Magufuli na Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana baada ya kusikiliza kwa kina kero na malalamiko ya kiuchaguzi ya wanachama wa CCM.

Akifafanua kuhusu suala hilo, alisema baada ya kusikiliza malalamiko hayo, Dk Magufuli alimuelekeza Kinana kuchukua hatua na kwa mamlaka aliyopewa, ameagiza kufutwa na kurejewa upya hivyo wanachama na viongozi wanatakiwa kufuata maagizo hayo.

Alizitaja kata hizo ambazo ni 20, ni za Mkoa wa Dar es Salaam na nafasi zinazotakiwa kurejewa katika mabano ni Kata ya Buguruni (Mwenyekiti na Katibu), Kata ya Liwiti (Katibu), Kata ya Kariakoo (Mwenyekiti, Katibu na Katibu Mwenezi), Kata ya Manzese (Mwenyekiti, Katibu na Katibu Mwenezi), kata za Makuburi, Mabibo na Kigamboni.

Nyingine ni Kiburugwa, Mchafukoge, Gerezani, Segerea (Mwenyekiti na Katibu), Pugu Stesheni (Mwenyekiti, Katibu na Katibu Mwenezi), Kata ya Mianzini, Kata ya Pugu (Katibu Mwenezi), Kata ya Ndugumbi, Kata ya Kilungule, Kata ya Makumbusho, Kata ya Kitunda (Katibu na Katibu Mwenezi), Kata ya Ukonga na Kata ya Msasani.

Chanzo: Habarileo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents