Habari

DC Iringa Mohamed Moyo, amuokoa binti aliyekuwa akibakwa na baba yake zaidi ya miaka 10

Mkuu wa wilaya ya Iringa Mohamed Hassan Moyo akiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Iringa walipomtembelea binti ambaye amekuwa akibakwa na baba yake mzazi  kwa zaidi ya miaka kumi(10)

Mkuu wa wilaya ya Iringa Mohamed Hassan Moyo amemuokoa mwanamke aliyekuwa akibakwa na baba yake kwa zaidi ya miaka kumi katika kijiji cha Mgama kitongoji cha katenge B baada ya kupokea taarifa ya kitendo hicho kutoka kwa wananchi wa kijiji hicho kwenye mkutano wa hadhara wa kusikiliza kero za wananchi wa vijiji vya wilaya hiyo.

Akiwa kwenye mkutano wa hadhara wa kusikiliza kero za wananchi wa katika kijiji Mgama ndipo lilipoibuka swala hilo baada ya mwananchi kufikisha lalamiko hilo kwa njia ya barua kwa mkuu wa wilaya juu ya tuhuma hizo kwenda kwa bwana Pancras Kiyeyeu ambaye ni baba ya mtoto huyo.

Baada ya kupokea barua hiyo mkuu wa wilaya kwa kushirikiana na kamati ya ulinzi na usalama walifunga safari hadi kwenye nyumba ambayo bwana Pancras Kiyeyeu anaishi na kumkuta binti huyo ambaye inaelezwa amekuwa akibakwa na baba yake.

Akizungumza mbele ya mkuu wa wilaya pamoja na kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya ya Iringa,binti huyo alikiri kufanyiwa kitendo hicho na baba yake mara kwa mara kwa kutumia nguvu na maneno ya kumtishia kumuua endapo ataongea kwa watu wengine.

Binti huyo alisema kuwa amekuwa akibakwa mchana na usiku na baba yake kwa zaidi ya miaka kumi hadi kumpelekea kupata ugojwa na kuanguka anguka(kifafa) na kusababisha kuathirika kisaikolojia ambako kumepelekea kudhohofisha afya ya binti huyo.

Wakitoa ushuhuda huo baadhi ya ndugu na majirani wa mzee Kiyeyeu walisema kuwa kumekuwa na taarifa hizo mara kwa mara jambo lilopelekea kumpeleka mzazi huyo kwa mwenyekiti wa Kitongoji cha Katenge B ambaye alifanikiwa kulimaliza kwa ngazi ya kifamilia ambapo ni kinyume na sheria za nchi.

Walisema kuwa mzazi huyo imekuwa tabia yake kwa miaka mingi kwa sababu kumekuwepo kwa malalamiko ya siku nyingi lakini yamekuwa hayafanyiwe kazi na uongozi wa kitongoji cha Katenge B na kusababisha mzee huyo kuwa huru na kuendelea kutenda vitendo hivyo kwa ndugu zake na watoto wake.

Mara baada ya kusoma barua na kupata maelezo ya binti aliyebakwa,majirani na ndugu zake wa mzee kiyeyeu,mkuu wa wilaya ya Iringa Mohamed Hassan Moyo alisema kuwa kitendo cha unyanyasi wa kijinsia alichofanyiwa binti huyo hakikubariki katika jamii yeyote hasa hasa katika wilaya hiyo.

 Moyo alisema kuwa uzalilishaji aliofanyiwa binti huyo haukubariki hata kidogo kutokana na wananchi wengi wa kitongoji hicho kulifahamu jambo hilo na kuliacha bila kulichukulia hatua kali za kisheria wakimuacha binti huyo kunyanyaswa kijinsia na baba yake.

Alisema kuwa ameliagiza jeshi la polisi wilaya ya Iringa kuhakikisha watuhumiwa wote wanakamatwa ndani ya masaa ishirini na nne (24) na kufikishwa mahakamani mara moja kwa kuwa ushahidi kwa kiasi kikubwa umekamilika mara baada binti na majirani kukiri kutokea kwa kitendo hicho.

Moyo alitoa onyo kali kwa wazazi na wananchi ambao wanafanya vitendo hivyo watachukuliwa hatua kali za kisheria

Mara baada ya agizo la mkuu wa wilaya ya Iringa kwa jeshi la polisi wilaya ya Iringa, Jeshi hilo limefanikiwa kuwatia mbaroni watu wawili akiwemo Pancras Kiyeyeu 62 mkazi wa Kijiji Cha Mgama Wilayani humo kwa tuhuma za kumbaka nakumtendea ukatili wa aina mbalimbali Binti yake anayesumbuliwa na ugonjwa la kifafa uliodhohifisha Afya yake.

Mtuhumiwa mwingine ni Mendilad Kitime mwenye umri wa miaka 44 ambaye ni mwenyekiti wa Kitongoji Cha Katenge B kilichopo katika kata Hiyo akidaiwa kutochukua hatua za kisheria kwa kuficha uhalifu huo hivyo akishiriki kuruhusu Binti huyo kuendelea kutendewa ukatili huo na baba yake mzazi kinyume na sheria za nchi zinavyotaka.

Aidha kulingana na hali ya afya ya binti huyo anayedaiwa kutendewa ukatili huo kuonekana kudhohofika zaidi, mkuu wa Wilaya ya Iringa ameagiza uongozi wa kata kumfikisha kwa wataalam wa afya ili afanyiwe uchunguzi na kupatiwa matibabu ya haraka.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents