Kamati kuu ya chama tawala ANC imekutana kwa majadiliano yatakayoamua kuhusu hatma ya rais Cyril Ramaphosa anayeandamwa kwa tuhuma za rushwa
Viongozi wa ngazi za juu ndani ya chama tawala nchini Afrika Kusini ANC wako kwenye mazungumzo yaliyoanza Jumatatu kujadili hatma ya rais Cyril Ramaphosa madarakani.
Kikao cha ANC kinafanyika wakati JumanneĀ bunge linatarajiwa kupiga kura katika hatua ambayo inaweza kumuondowa madarakani. Mkutano huo utatowa maamuzi ikiwa Ramaphosa anabakia kuwa mwenyekiti wake au anapaswa kuondolewa.
Mwishoni mwa juma rais Ramaphosa alisisitiza kwamba hatojiuzulu baada ya jopo maalum kutoa ripoti yake kuhusu tuhuma za kumuhusisha kiongozi huyo na kadhia ya kuficha tukio wizi wa fedha uliotokea baada ya makaazi yake ya shambani kuvamiwa na kuvunjwa na majambazi. Hata hivyo ukweli wa mambo ni kwamba mustakabali wa kisiasa wa rais huyo bado haujulikani.
Siku ya Jumatatu Ramaphosa alionekana akiwasili kwenye eneo la mkutano wa kamati kuu ya chama cha ANC,NEC ambayo ndio chombo chenye maamuzi ya mwisho ya chama,lakini aliondoka muda mfupi baadae akionekana mwenye kutabasamu na kuwapungia mkono waandishi habari.