IGP Sirro aahidi kiama cha wauaji Kibiti
Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Tanzania (IGP), Simon Sirro amesema siku zinahesabika kwa wahalifu wote waliojificha mkoani Pwani ambao wamekuwa wakifanya matukio ya uhalifu ikiwa pamoja na kufanya mauaji kwa baadhi ya viongozi na askari polisi nchini.
IGP Sirro amesema yeye sio mzungumzaji sana bali ni mtu wa vitendo na muda sio mrefu atatoa majibu ya mauwaji hayo kwa vitendo.
“Si kawaida yangu kusema sema ila muda si mrefu nitatoa majibu ya mauaji ya Pwani kwa vitendo,” amesema IGP Simon Sirro jana alipokuwa katika ukumbi wa Police Officer’s Mess, Oysterbay jijini Dar es Salaam wakati akikabidhiwa magari manne na kampuni ya kichina ya Great Wall Motors and Haval na kudai kuwa magari hayo yatasaidia kupambana na uhalifu nchini.
Mpaka sasa watu 35 wameripotiwa kupoteza maisha mkoani Pwani kwa kuuliwa na watu wasiojulikana huku wengine kadhaa wakiwa wakijeruhiwa .