Mabala apambania Kiswahili Sekondari
Baada ya maoni kuwa mengi mitandaoni kuhusu kutumia lugha ya Kiswahili shule za Sekondari, Mwandishi wa vitabu, Richard Mabala amesema anakazia kauli yake kwa kuwa lengo la elimu ni uelewa na si vinginevyo.
Katika kauli yake aliyoitoa jana, Oktoba 4, 2021, wakati akizungumza kwenye kipindi cha Supa Breakfast cha East Africa Radio, Mabala alisema kwamba Kiingereza kifundishwe vizuri zaidi kama somo ili kieleweke kwa ufasaha na si masomo kufundishwa kwa kutumia lugha hiyo.
Leo,5, Oktoba kupitia ukurasa wake, Mabala amesema ” Narudia lengo la elimu ni watu wapanue uelewa na stadi. Hufanyika vizuri kama wanaelewa lugha inayotumika. Wanafunzi walio wengi sana hawatavuka Kidato cha 4 hivyo wanahitaji kupata uelewa na stadi za kutosha kabla ya hapo
“Kutumia kiingereza kama lugha ya kufundisha si njia bora ya kuifundisha, hasa kama hawana kiingereza cha kutosha na hawakai katika mazingira ya kuweza kupatauzoefu wa kutosha. Watajua kiingereza vizuri zaidi kwa kufundishwa hatua kwa hatua na walimu walioandaliwa vizuri kufanya hivyo,” amesisitiza
aidha Nguli huyo amesisitiza kwamba tafiti karibu zote, tangu miaka ya 80 wakati shule bado zilikuwa chache zinaonesha kwamba wanafunzi walio wengi hawakuwa na kiingereza cha kutosha kukitumia kama lugha ya kufundishia.
BY: Fatuma Muna