Burudani

MCT yaiadhibu Times FM, baada ya mtangazaji wake kumshambulia hewani msanii wa Taarab

Kamati ya Maadili ya Baraza la Habari Tanzania (MCT) imekitaka kituo cha Radio Times FM ya Dar es salaam kuomba radhi mfululizo siku tatu na kumlipa tsh 500,000 msanii wa Taarab, Karya Temba baada ya mtangaji wake, Dida kupitia kipindi cha ‘Mitikisiko ya Pwani’ kumshambulia binafsi msanii huyo.

CIMG5204

Kamati imesema mtangazaji Hadija Shaibu maarufu Dida aligeuza kipindi anachorusha redioni hapo kuwa cha ugomvi binafsi kati yake na mlalamikaji ambaye ni Karya na kwamba alichochea wasikilizaji kutuma meseji za kejeli kwa mlalamikaji jambo ambalo sio lengo la usajili wa kituo hicho.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Jaji mstaafu Thomas Mihayo wakati akifafanua juu ya malalamiko ya msanii huyo akidai kipindi hicho kilimdhalilisha na kumharibia sifa kama mwanamuziki.

Jaji Mihayo alisema baada ya kamati kusikiliza pande hizo mbili, inaagiza redio hiyo kumwomba radhi mlalamikaji kupitia kipindi hicho katika vipindi vitatu mfululizo kuanzia Februari 5 na maudhui ya radhi hiyo yataridhiwa na MCT.

Alisema kituo hicho, pia kimlipe mlalamikaji Sh 500,000 kama gharama za kutayarisha malalamiko na kimuandikie barua ya kumwomba radhi ndani ya wiki moja kuanzia jana na nakala kutumwa MCT. Katika shauri hilo namba 28, 2013, Temba analalamika kushambuliwa, kukashifiwa na hata kubaguliwa na mtangazaji huyo katika kipindi chake cha Mitikisiko ya Pwani anachokirusha redioni hapo.

Vile vile Kamati hiyo imesema redio hiyo ilikiuka maadili ya utangazaji kwa kurusha kipindi kinachoshutumu watu kwa kutumia kabila lao na kilikuwa na maudhui ya udhalilishaji wa kijinsia, kinyume cha maadili na kanuni bora za uanahabari.

Source: Habari Leo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents