Mr. Nice na Dkt. Shika ni wale wale – Dudu Baya
Baada ya Mr. Nice kudai ana uwezo wa kumpatia msaada wa kifedha Dudu Baya, hatimaye Dudu Baya amemjibu.
Dudu Baya amesema Mr. Nice amehathirika kisaikolojia baada ya kushika fedha nyingi kisha zikatoweka na kueleza kuwa msanii huyo hana tofauti na Dkt. Louis Shika.
“Hali ya Mr. Nice ni mbaya sana kiafya hadi kiuchumi, kwa hiyo amehathirika kisaikolojia ndio maana mtu kama huyu anaota yale maisha yake ya umaarufu kipindi kile na mpunga alioupiga kipindi kile na ile pesa yote ikayeyuka” amesema Dudu Baya.
“Kwa hiyo vitu vya kuropoka anataka kunisaidia siwezi kumshangaa kwa sababu hata Dkt. Shika alikuwa na hela Urusi lakini hizo hela hazipo na bado anaziota anajiona kama bado anazimiliki zile pesa, kwa hiyo Mr. Nice na Dkt. Shika ni wale wale” amesisitiza.
Umaarufu wa Dkt. Shika umekuja baada ya kujitokeza katika mnada wa kuuza nyumba za Lugumi ambapo Dk. Shika aliahidi kununua nyumba hizo kwa thamani ya Sh bilioni 2.3 lakini alishindwa kulipia asilimia 25 ya fedha hizo ambazo ni shilingi milioni 800, kisha kudai anangojea fedha zake kutoka nchini Urusi.