SADC kupeleka wanajeshi mpaka wa Msumbiji na Tanzania
Viongozi wa Jumuiya ya maendeleo ya Kusini mwa Afrika, (SADC) wamekubali kupeleka wanajeshi kusaidia kudhibiti uasi unaofanywa na kikundi cha kigaidi kinachofanya mauaji na kusababisha taharuki kaskazini mwa Msumbiji kwa kipindi cha miaka mitatu sasa.
Hata hivyo, haijafahamika kwa kina kuhusu kikosi hicho na muda ambao kitatumia kukabiliana na Magaidi hao, lakini mapema mwaka huu, iliripotiwa kuwa SADC inatarajiwa kutuma wanajeshi 3,000 nchini humo.
Mwenyeji wa mkutano huo, Rais Filipe Nyusi wa Msumbiji ambaye pia ni Mwenyekiti wa sasa wa Jumuiya ya SADC aliitisha mkutano huo ili kuomba usaidizi wa marais wenzake kuhusu kitisho cha magaidi hao, ambao wamekuwa wakiendesha mashambulizi katika jimbo la Capo Delgado,kaskazini mwa Msumbiji
Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya SADC, Stragomena Pax, amesema marais hao wamekubaliana kupeleka kikosi cha pamoja cha Jumuiya hiyo nchini Msumbiji ili kuimarisha usalama wa eneo hilo, huku wakitoa wito wa kupewa msaada wa Kimataifa katika mapambano yake dhidi ya ugaidi.
Wapiganaji wa kigaidi wameshutumiwa kwa kufanya mauaji ya kikatili tangu mwaka 2017 kwa kufanya uvamizi wa vijiji na miji maeneo ya mpaka kati ya Msumbiji na Tanzania
By- BAKARI WAZIRI