Spika Ndugai akiri changamoto wabunge wapya
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai amekiri kuwepo kwa wabunge wengi wapya katika bunge hilo imekuwa ni moja ya changamoto katika uelewa wa majukumu yao kutokana na wengi kutozifahamu vyema kanuni za bunge.
Mhe. Ndugai anabainisha changamoto hiyo mbele ya wajumbe kutoka nchi za jumuiya ya Nordic pamoja na washirika wa maendeleo kutoka shirika la maendeleo la umoja wa mataifa (UNDP) ambao ni wafadhili wa mradi wa kuwajengea uwezo wabunge.
“Tulikuwa tunatumia nafasi hii kuwashawishi wakubali kuendelea kutusaidia katika kuwezesha shughuli zetu za bunge ili ziweze kwenda vizuri zaidi, hasa katika upande wa kujenga uwezo, na asilimia kubwa ya wabunge wetu ni wapya na ni vijana na wengi hawana uzoefu mkubwa wa kufanya kazi serikalini au mahali pengine,”alisema Ndugai.
“Kwahiyo kupitia semina hizi zinasaidia sana semina za vijana, wabunge vijana, wabunge kina mama na makundi mbalimbali ya wabunge kupitia uwezesho huo inatusaidia sana kwa mbunge mmoja mmoja au makundi ya wabunge kufanya kazi yao ya kibunge vizuri zaidi”.
BY: EMMY MWAIPOPO