Habari

TRA yakamata akaunti za Kampuni ya Sahara Media Group kwa kushindwa kulipa deni la Sh4 bilioni

Mamlaka ya Mapato Tanzania(TRA) imekamata akaunti za Kampuni ya Sahara Media Group ambayo inamiliki vituo vya habari vya Star TV, Kiss FM pamona Radio Free Africa kwa kushindwa kulipa deni la Sh4 bilioni kama kodi iliyopaswa kulipwa na kampuni hiyo.
7
Mkurugenzi wa Sahara Media Group, Mh.Dkt.Antony Diallo

Taarifa zilizosambaa kupitia mitandao ya kijamii zimeeleza kuwa akaunti zote za kampuni hiyo zimefungiwa mpaka pale watakapolipa deni hilo, lakini kampuni hiyo imetoa ufafanuzi.

Ujumbe huo uliongeza kuwa kampuni hiyo imefikishwa mahakamani na benki moja hapa nchini kwa madai ya kutaka kulipwa Sh600 milioni, baada ya kuingia makubaliano ya kulipa wafanyakazi wake mishahara pamoja na mikopo lakini mpaka sasa imeshindwa kurejesha fedha hizo.

Hata hivyo, akizungumzia suala hilo mwenyekiti mtendaji wa kampuni ya Sahara, Anthony Diallo alikiri mamlaka hiyo kufungia akaunti ya kampuni yake.

Diallo ambaye ndiye mmiliki wa kampuni hiyo alisema ni akaunti moja tu iliyofungiwa na kwamba anaamini baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na mamlaka hiyo watafikia muafaka ili biashara ziendelee kama kawaida.

“Tutalimaliza hakuna kitakachoenda mrama,” alisisitiza Diallo ambaye aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwamo nafasi ya Waziri wa Maliasili na Utalii na Naibu Waziri wa Maji, Maendeleo ya Mifugo katika Awamu ya Nne chini ya Rais mstaafu Jakaya Kikwete.

Amesema deni la TRA linatokana na kodi iliyopatikana baada ya ukaguzi wa vitabu kwa miaka mitatu. “Ni ukaguzi wa kawaida hufanyika kama taratibu. Sasa kwa sababu ya kuhamisha matangazo yetu kutoka analojia kwenda digitali ilibidi tukope benki, ujenzi na kumaliza mradi imechukua miaka mitatu. Wakati wote tumekuwa tukilipa riba benki na zinazobaki toka mauzo ya matangazo tunalipa mishahara, umeme na malipo ya kodi za kawaida,”alisema.

“Ni kawaida ila wamefanya hatua za kutuaibisha tu. Kampuni yetu ya ving’amuzi ni ya Kitanzania na mapato yote yanaingia nchini wakati kampuni nyingine kubwa zote ni za kigeni kutoka China, Afrika Kusini, Mauritius na Kenya! Ukweli sisi tunahitaji kusaidia nchi kiuchumi na kutuharibia ni hasara kwa nchi.”

Hata hivyo, baadaye jioni mwenyekiti huyo aliliambia Mwananchi kuwa tayari wamefanya mazungumzo na mamlaka hiyo na kukubaliana jinsi gani watalipa deni hilo.

“Tumezungumza nao wametuelewa na kutupa namna ya kulipia, sisi ni wafanyabiashara ni lazima tufuate taratibu za biashara ili biashara yetu iende vizuri,”.

Alipoulizwa kuhusu taarifa hizo, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi, Richard Kayombo aliomba apewe muda aulize kutokana na yeye kuwapo safarini.

“Taarifa hizo sina kwa sababu nipo safarini Ngorongoro naomba niulizie ofisini nitakurudia nikupe jibu,” alisisitiza Kayombo.


Source: Mwananchi

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents