Afya

Je, upo tayari kuambukizwa ugonjwa wa kifaduro kwa Tsh milioni 10?

Ukistaajabu ya Musa utaona ya Firauni, Hii sio hadithi tena bali ni ukweli kama upo tayari kulipwa kiasi cha Milioni 10 za Kitanzania kwa kuambukizwa ugonjwa wa kifaduro/Dondakoo kwa ajili ya utafiti wa kisayansi basi kazi inabaki kuwa ni kwako.

Ill man

Watafiti kutoka chuo kikuu cha Southampton cha nchini Uingereza wamesema wapo tayari kutoa kiasi hicho cha pesa ili kutatua changamoto wanayoipata katika masomo yao ya utafiti wa kutafuta chanjo ya ugonjwa huo hatari kwa watoto.

Wataalamu na Madaktari bingwa kutoka chuoni hapo wanataka kutengeneza chanjo bora ili kuwalinda watoto na watu wazima ambao wapo hatarini kuambukizwa ugonjwa huo.

Jopo hilo kutoka mjini Southampton linataka kuwaambukiza watu walio na afya nzuri kwa kuwawekea puani viini vinavyosababisha maambukizi hayo na kuwachunguza kisha kufanya utafiti wa utengenezaji wa chanjo ya ugonjwa huo.

Kwa mujibu wa mtandao wa Daily Mirror taarifa zimeeleza kuwa watu wote watakaojitokeza watapewa huduma zote muhimu za usafiri kwa wale watakaokuwa nje ya Uingereza, Malazi, Chakula na masuala ya saikolojia kwa siku zote 17.

Moja ya watafiti walio kwenye jopo hilo, Prof. Robert Read amesema malipo ya Milioni 10 ni kwa ajili ya muda wa watu hao watakaojitolea na idadi ya watu wanaohitajika ni 35 na mpaka sasa wamepata watu 16 tuu.

Prof Rob Read
Prof. Robert Read

Watu hao watakaojitokeza watakuwa wanakusanya makamasi na makohozi yao kwenye kisanduku maalumu kwa muda wote kwa ajili ya shughuli za utafiti.

Hata hivyo watafiti hao wametoa tahadhari kuwa kwa wote watakaojitolea kuambukizwa viini hivyo watakuwa wagonjwa kwa siku 17 na umri wanahitajika watu wenye umri kati ya miaka 18-45  na wakubali kutengwa na jamii kwa siku zote 17 wtakazokuwa wanaumwa.

Uingereza ni moja ya mataifa barani ulaya yanayokabiliwa na vifo vingi vya watoto vinavyotokana na ugonjwa wa Kifaduro ambapo kuanzia mwaka 2012 hadi sasa kuna kesi ya vifo vya watu 8.

Kama bado haujui ugonjwa wa kifaduro unavyoambukizwa na dalili zake Bonyeza HAPA na wale ambao wapo tayari kujitolea kufanyiwa utafiti unaweza ukawasiliana na Mkuu wa Idara ya tafiti chuoni hapo kwa Email hii [email protected] .

By Godfrey Mgallah

 

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents