CHADEMA yapata pigo, Yakimbiwa na mjumbe wa bodi ya wadhamini
Aliyewahi kugombea Ubunge wa Jimbo la Ilala kwa tiketi ya CHADEMA mwaka 2015, Muslim Hassanali leo Jumanne Januari 9, 2018 ametangaza kukihama cha hicho na kujiunga CCM.
Hatua hiyo ya Hassanali inakuja katika kipindi ambacho wanasiasa wengi wa vyama vya upinzani wakiwemo Wabunge na Madiwani wamekuwa wakivihama vyama vyao na kukimbilia CCM.
Kiongozi huyo ambaye pia alikuwa mjumbe wa bodi ya wadhamini wa CHADEMA, amepokelewa na Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Philip Mangula akiwa na viongozi wengine wa CCM katika ukumbi wa Checkpoint Pugu jijini Dar es salaam.
“Nimeikosoa serikali vya kutosha sasa nimeona ni wakati wa kushirikiana nayo kutekeleza yale ambayo nimekuwa nikiyasema kwa maslahi ya Watanzania,“amesema Muslim Hassanali.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Hamphrey Polepole amesema Hassanali ameomba kwa muda mrefu hivyo wameona hakuna jinsi zaidi ya kumruhusu.