Habari

Halmashauri zatakiwa kurejesha fedha za mikopo ya KKK kupitia vyanzo vingine

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Geophrey Pinda ameziagiza halmashauri zote nchini zilizokopeshwa fedha kwa ajili ya programu ya kupanga, kupima na kumilikisha ardhi (KKK) kutafuta vyanzo vingine vya fedha kwa ajili ya kuzirejesha ili halmashauri nyingine zinufaike na mkopo huo.

Pinda alitoa kauli hiyo leo tarehe 20 Machi 2024 mkoani Shinyanga wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) ilipotembelea na kukagua utekelezaji mradi wa Uimarishaji Usalama wa Milki za Ardhi nchini (LTIP) katika katika Kata ya Ibadakuli.

Kauli ya Pinda inafuatia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kutaka kujua hatua zinazochukuliwa na wizara baada ya kuelezwa kuwa, halmashauri ya manispaa ya Shinyanga ni mojawapo ya halmashauri zilizopewa fedha hizo ambapo ilipata shilingi bilioni 1.055 na kushindwa kuzirejesha kwa mujibu wa makubaliano.

“Halmashauri zote nchini zitafute vyanzo vingine kwa sababu hili jambo limeulizwa mara kadhaa na kama wizara tumeeleza mkakati tunaoenda nao” alisema Pinda.

Kwa mujibu wa Pinda, wizara yake kwa sasa haiangalii tena malengo ya mradi katika kupata fedha na badala yake inaenda mbali zaidi ili halmashauri zitumie vyanzo vingine kulipa deni na wakati huo halmashauri hizo zikitumia vyanzo vingine kupata fedha.

Ameitaja halmashauri ya wilaya ya Chalinze iliyopo mkoa wa Pwani kuwa, itakuwa halmashauri ya mfamo kwa kuwa tayari imeonesha nia ya kulipa deni inalodaiwa la shilingi Bilioni 2.5 kupitia vuanzo vingine.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) Japhet Hasunga amesema kamati yake itaenda kulishuggulilia suala hilo la kusuasua kwa halmashauri kurejesha mikopo ya programu ya KKK na kuona namna ya kulishauri Bunge juu ya suala hilo.

Ameeleza kuwa, msingi mkubwa wa serikali kutenga fedha za mkopo kwa ajili ya mradi wa KKK ni kutaka programu hiyo kuwa endelevu na mwisho wananchi waweze kupatiwa hati milki za ardhi.

“Tunataman kila kipande cha ardhi yetu ipangwe, ipimwe na kumilikishwa na ikianyika hivyo ndiyo tutaona thamani ya ardhi yetu” alisema Mhe, Hasunga.

Akielezea kuhusu mradi wa uboreshaji usalama wa milki za ardhi (LTIP) uliotembelewa na Kamati hiyo ya PAC, mhe, Pinda amesema mradi huo katika halmashauri ya manispaa ya Shinyanga ulianza oktoba 2024 kwa lengo la kurasimisha vipande vya ardhi 20,000 ifikapo juni 30, 2024.

Amesema, hadi sasa vipande vya ardhi 21,850 vimetambuliwa , vipande 7,175 vimepangwa na viwanja 1,315 vimepimwana kwa ujumla kazi hiyo imetekelezwa kwa asilimia 51 na kazi ikiendelea.

Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP) ulibuniwa na wizara ya ardhi ili kutatua changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikiikabili sekta ya ardhi kwa muda mrefu. Changamoto hizo ni pamoja na mabadiliko ya teknolojia katika utekelezaji wa kazi za sekta na utoaji huduma za ardhi, kukosekana kwa miundombinu wezeshi ya TEHAMA katika ofisi za ardhi pamoja na kasi ndogo ya upangaji, upimaji na umilikishaji ardhi.

Written by Janeth Jovin

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents