Rais huyo wa zamani wa Kenya alitowa kauli hiyo usiku wa Jumatatu (Novemba 14) mjini Kinshasa wakati wa mkutano na waandishi wa habari alioufanya baada ya kuzungumza na viongozi mbalimbali, akiwemo Rais Felix Tshisekedi, Tume ya Umoja wa Mataifa (MONUSCO) pamoja na wanadiplomasia.
Kenyatta alikuwa nchini Kongo kwa lengo la kukusanya maoni tofauti ya kutafuta amani na usalama katika eneo la mashariki mwa nchi hiyo linalokumbwa na makundi yanayomiliki silaha.
Mjumbe huyo maalum wa Jumuiya ya Afrika Mashariki aliahidi kuendeleza kazi hiyo na Rais Joao Lourenço wa Angola ili kufikia lengo, lakini akisisitiza kwamba ni lazima iwepo heshima kwa serikali ya Kongo, katiba na mamlaka.
“Tunayo serikali iliyochaguliwa ambayo uhalali wake lazima tuulinde. Pili, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ina katiba ambayo lazima iheshimiwe na hatimaye, kuheshimiwa kwa mamlaka ya eneo la Kongo.” Alisema.