Habari
Malawi: Mahakama yafuta matokeo ya uchaguzi wa Rais, yaipa tume siku 150
Mahakama ya Katiba ya Malawi imeyafuta matokeo ya uchaguzi wa rais wa Mei 2019, uliompa ushindi Rais Peter Mutharika.
Mahakama ya Katiba ya Malawi imeyafuta matokeo ya uchaguzi wa rais wa Mei 2019, uliompa ushindi Rais Peter Mutharika.
Akitoa uamuzi wake hapo jana, Jaji Healey Potani alisema ingawa chaguzi zote zina mapungufu, uchaguzi uliopita ulighubikwa na hitilafu za kimfumo zilizokithiri kiasi cha kuweza kubadilisha matokeo.
Kwa mujibu wa shirika la habari la DW, Mahakama hiyo ilisema matokeo ya uchaguzi huo yamebatilishwa, na kuitaka tume ya uchaguzi kuandaa uchaguzi mwingine katika muda wa siku 150.
Katika uchaguzi huo, Rais Mutharika aliyekuwa akiwania muhula wa pili alipata ushindi mdogo wa asilimia 38, huku mpinzani wake mkuu Lazarus Chakwera akikusanya asilimia 35.
Aliyekuwa makamu wa rais, Saulos Chilima alikuja katika nafasi ya tatu na asilimia 20. Huu ni uchaguzi wa kwanza kubatilishwa na mahakama nchini Malawi, tangu taifa hilo lilipopata uhuru mwaka 1964.
Usalama umeimarishwa kote nchini humo baada ya uamuzi huo wa Mahakama.