Mgomo wapelekea shughuli za usafiri kusimama, mamlaka zaagiza wakazi wa Paris kufanya kazi nyumbani
Shughuli za usafirishaji zimesimama jijini Paris, wakati vyama vya wafanyakakazi vikiandamana kupinga mageuzi makubwa ya pensheni yaliyotangazwa na serikali ya rais Emmanuel Macron.
Kampuni ya usafiri wa umma, RATP imesema njia 10 za reli zimefungwa pamoja na nyingine nyingi na kusababisha kadhia kubwa. Usafiri wa mabasi na treni za chini pia umeathirika.
Ujumbe ulioandikwa kwa Kifaransa na Kiingereza na kuwekwa kwenye vituo vya usafiri ulionya abiria kuhusu mgomo huo, ambao ni mkubwa zaidi tangu maka 2007.
Treni ambazo ziliendelea kuhudumu zilikuwa chache tofauti na ilivyo kawaida, wakati mamlaka zikiwataka watu wanaoishi Paris kufanya kazi wakiwa nyumbani ama kutafuta usafiri mbadala.
Rais Macron anataka kufanya mageuzi hayo kwa hoja kwamba yatafanya pensheni kwa umma kuwa sawa, na kuahidi umri wa kustaafu kusalia miaka 62, na masharti mapya yanaweza yakawahamasisha watu kufanya kazi muda mrefu zaidi kabla ya kustaafu.