Bongo5 Makala

Mtoto wa rais wa Angola, ndiye mwanamke tajiri zaidi Afrika, ana utajiri wa $bil.3

Isabel Dos Santos ni mtoto wa kwanza wa rais José Eduardo dos Santos wa Angola aliyezaa na mke wake wa kwanza, Tatiana Kukanova.

Ni mrembo, msomi na tajiri haswaaa. Alisoma kwenye shule ya serikali jijini Luanda, ambapo wakati huo hakukuwa na shule binafsi. Inasemekana licha ya kuwa mtoto wa familia bora, Isabel alikuwa mnyenyekevu na mtu wa watu na kipenzi chao.

Baba yake alipata urais 1979, ambapo Isabel na mama yake waliyekuwa tayari wameachana na mumewe walihamia London, Uingereza.

Kwa mujibu wa gazeti la mwaka 1991 ka Uingereza, Isabel alisoma kwenye shule ya St Paul jijini London. Alisomea masomo ya ukandarasi wa umeme na biashara kwenye chuo cha King’s College.

Huko kwao Angola, akiwa na miaka 24, biashara yake ya kwanza ilikuwa ni mgahawa uitwao Miami Beach. Haukuwa na mafanikio kutokana na utaratibu mbovu na wafanyakazi wazembe. Baadaye alihamia kwenye biashara ya kukusanya uchafu ambayo nayo ilikwenda mrama.

Kwa mujibu wa The Guardian, kwa sasa Isabel ana asilimia 28 za hisa kwenye kampuni kubwa la habari za Ureno, Zon ambazo zina thamani ya dola milioni 385. Pia anamiliki asilimia 19.5% kwenye benki ya Kireno, Banco BPI, zenye thamani ya dola milioni 465 huku akiwa na asilimia 25 kwenye benki hiyo tawi la Angola zenye thamani ya dola milioni 160.

Kwa kuongeza ana hisa 25% kwenye kampuni ya simu ya Angola, Unitel. Mwaka 2003 Dos Santos aliolewa na Sindika Dokolo, mfanyabiashara wa Congo na mtoto wa Sanu Dokolo, mwanzilishi wa Bank of Kinshasa. Wakiwa na watoto watatu, wapenzi hao hugawa muda wao kuishi Luanda, London, Lisbon na Johannesburg, ambako Dokolo ana ndugu.

José Eduardo dos Santos, Angola's president, left, and daughter Isabel dos Santos in the second row
Rais wa Angola, José Eduardo dos Santos akiwa na mke wake wa tatu Ana Paula dos Santos. Nyuma yao ni Isabel dos Santos (anayepiga makofi) akiwa na mume wake Sindika Dokolo mjini Luanda.

Isabel huongea lugha nyingi lakini hapendi kuongea na vyombo vya habari kama baba yake.Hadi sasa, akiwa umri wa miaka 40, mwanamke huyo ana utajiri wa dola bilioni 3 unaomfanya si tu awe mwanamke tajiri zaidi Afrika, bali pia kijana tajiri zaidi katika bara hilo.

Hata hivyo jarida la Forbes limefanya uchunguzi wa muda mrefu kutaka kufahamu iwapo utajiri wake ni wa halali.
Lilibaini kuwa ni utajiri wa baba yake uliopandikizwa kwake.

Kama rais huyo mwenye miaka 71 akipinduliwa, anaweza kudai mali zake kwa binti yake. Akifariki akiwa madarakani, utajiri huo atabaki nao yeye, Isabel. Isabel anaweza kuamua, kama akiwa na roho nzuri kugawana na wadogo zake saba wa mama mwingine ama kuwapiga chini. Ndugu hao wanajulikana nchini Angola kwa kudharauliana wao wenyewe.

“Ni ngumu kuhalalisha utajiri huo,” Waziri Mkuu wa zamani wa Angola Marcolino Moco aliiambia Forbes.

“Hakuna shaka kuwa ni baba yake ndiye aliyezalisha utajiri huo,” alisema.

Source: Forbes na The Guardian

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents