‘Nashukuru tunapumua’ asema Dk Bilal baada ya kunusurika kifo kwa ajali ya helikopta akiwa na Kova na Magufuli
![](https://bongo5.com/wp-content/uploads/2014/04/DrMohamedGharibBilal1.jpg)
Makamu Rais Dk Mohamed Gharib Bilal amesema anamshukuru Mungu kwakuwa yupo hai na anapumua baada ya jana kunusurika kifo kutokana na ajali ya helikopta.
Helikopta hiyo baada ya kuanguka
Dk Bilal, Waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Sadick Meck Sadick na Kamishna wa polisi kanda maalum ya Dar es Salaam, Suleimain Kova walinusirika kufa kutokana na helikopta hiyo kugonga ukuta na kuanguka wakati ikirudi nyuma ili kujiandaa kuruka kutoka kwenye uwanja wa ndege wa kikosi cha anga, Ukonga Dar es Salaam. Helikokta hiyo ilikuwa itumiwe na viongozi hao kukagua athari za mvua iliyonyesha weekend hii jijini Dar es Salaam, Pwani na Morogoro.
“Tulikuwa tunataka kuruka kuanzia saa tatu na nusu tuwe tumeingia hewani ili twende zetu moja kwa moja sehemu mbalimbali. Lakini bahati mbaya ndege wakati inarudi nyumba ikagonga ukuta na ikabidi ianguke,” DK Bilal aliwaambia waandishi wa habari.
“Namshurukuru mwenyezi Mungu kuwa sote tuliokuwemo kwenye ndege ile tumesalimika tuko salama tunapumua vizuri, tumeangaliwa vizuri na tunashukuru Mungu kuwa sote tupo katika hali nzuri. Japo baadhi yetu wawili walikuwa wamepata athari kidogo za michubuko ya kugongwa na chuma wakati ndege ile ilipoinamia upande mmoja wamepata michuko kidogo nao wameshashughuliwa na kila mmoja yupo katika hali nzuri,” aliongeza.