Habari

Ndalichako akabidhi ofisi kwa Waziri Mkenda

Aliyekuwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako leo Januari 13, 2022 amekabidhi ofisi kwa Profesa Adolf Mkenda ambaye ameteuliwa kuchukua nafasi hiyo na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan.

Wakati wa makabidhiano hayo, Waziri Mkenda amesema atatumia wataalam wa elimu walipo ndani na nje ya wizara ili kuwa na maamuzi yenye tija kwa nchi.

Waziri Mkenda amesema hayo leo Januari 13, 2022 jijini Dodoma wakati akikabidhiwa ofisi na aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo Profesa Joyce Ndalichako ambapo ameongeza kuwa katika uongozi wake hatatoa maamuzi juu ta sekta ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ubunifu bila ya kushauriana na wataalam husika katika sekta hiyo.

Profesa Mkenda amesema anafanya hivyo kwa kuwa Wizara hiyo inahitaji utulivu na siyo ya kubadilisha mambo ama kutoa matamko bila kuzingatia maoni ya wataalam kwani kufanya hivyo ni kuwachanganya wananchi.

“Kabla ya kufanya maamuzi yoyote katika elimu lazima kuwe na mijadala mipana iliyo huru kwa kutumia wataalamu wa ndani na nje ya wizara ili tuwe na maamuzi ya pamoja yenye tija,” amesema Prof. Mkenda

Waziri huyo ameendelea kuwasisitiza watumishi wa wizara hiyo na watalaam wa elimu *waliopo wizarani kutoa maoni walionayo, kufanya kazi kwa ujasiri, nidhamu na kujiamini na kwamba linapokuja suala la ubora wa elimu anawategemea.

Akizungumza katika hafla hiyo Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce Ndalichako amesema Wizara ya Elimu ni kubwa ambayo inashughulika na wananchi moja kwa moja na hivyo inahitaji umakini.

Amesema kati ya Miradi iliyoleta tija ni wa Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R) ambao katika awamu ya kwanza tu ambayo imekamilika mwezi Desemba 2021 umeacha alama kwa watanzania kwani umegusa kila kona ya nchi kwa kujenga miundombinu mbalimbali.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents