Burudani

Ni kweli ngoma haziendi bila kuwa na video au wasanii wanafanya ngoma za kawaida?

“Sasa hivi bila kuwa na video nzuri wimbo haufiki popote,” hii ni kauli ambayo nimekuwa nikiisikia sana kutoka kwenye vinywa vya wasanii wa Tanzania.

shutterstock_138386987

Kiukweli ni kauli yenye ukweli kwa mazingira yalivyo sasa. Na nadhani ni kwasababu mapinduzi ya teknolojia yaliyofanya matumizi ya simu yawe makubwa, yamewafanya mashabiki wengi wa muziki kuwa na uwezo wa muda wote kuangalia video kwenye simu zao. Watu hawategemei tena kusubiri kuona video za muziki kwenye TV tu.

Na ukweli ni kwamba siku hizi mashabiki wanapenda sana kuangalia kuliko kusikiliza tu. Hali hiyo imewafanya wasanii kuumiza vichwa sana kutengeneza video nzuri kwaajili ya ngoma zao.

Miaka ya nyuma, mambo hayakuwa hivyo. Video zilikuwa chache sana na pengine ni kwasababu hakukuwepo na waongozaji wengi wa video. Pamoja na hivyo, hits nyingi sana zilizaliwa. Kipindi hicho maproducer kama P-Funk, Master J, Mika Mwamba, Roy na wengine walitengeneza ngoma zilizosumbua mawimbi ya redio na kuingia kwenye vichwa vya watu bila hata kuwa na video.

Hits kibao za wasanii kama Juma Nature, Profesa Jay, Jay Moe, Ngwair, Mwana FA, AY na wengine hazikuwa na video lakini bado zilihit ile mbaya. Katika kipindi hiki ambacho uhakika wa mtu kuipata ngoma ni rahisi zaidi kuliko zamani, iweje tuamini kuwa wimbo hauwezi kufanya vizuri kama hauna si video tu, bali video nzuri? Yaani imefika wakati kama wimbo hauna video basi kuna nyota fulani zinatolewa au kwa lugha nyingine wimbo unakuwa na kasoro.

Mimi bado naamini kuwa wimbo unaweza ukahit na kuwa anthem bila hata ya kuwa na video na kutokana na kufanya kwake vizuri, kunakuwepo na demand kubwa zaidi kutoka kwa mashabiki ya watu kutaka video yake.

Wakati mwingine nahisi nyimbo zinashindwa kufanya vizuri si kwasababu hazina video bali ni za kawaida mno. Au wakati mwingine wasanii huumiza zaidi kichwa na kutumia gharama kubwa kufanya video nzuri kwa nyimbo za kawaida au mbaya. Yaani msanii anaingia studio kurekodi wimbo akimfikiria zaidi director wa video atakavyoifanya video hiyo bila kufikiria kwanza kutengeneza hit studio.

Na ndio maana wasanii wengi wapo radhi kumlipa producer shilingi lakini tano na kwenda kufanya video ya shilingi milioni 30 South. Wasanii hawaumizi tena kichwa kutengeneza nyimbo bora bali wanafikiria tu kutengeneza video bora ili nao waonekane MTV Base au Trace TV.

Ndio maana kuna nyimbo kibao zina video nzuri lakini hata hazikiki kitaa ni kwasababu ni mbovu. Na wengine wameishia kuwa na stress baada ya kutumia fedha nyingi kufanya video za nyimbo ambazo hazifiki popote. Ni sawa na kuupaka mafuta na manukato mwili wako bila kuoga.

Ngoma nyingi sana zinapigwa nusu nusu na hivyo kuhit yenyewe inakuwa jambo gumu. Hata kama ikiwa na video ya $20,000, itapotea fasta kwenye masikio.

Juzi nilikutana na Master J na nilimdadisi sana kuhusu utayarishaji wa muziki uliochezwa live. Nilimuuliza inagharimu kiasi gani kuchukua bendi kwa mfano Njenje au Inafrica na kumsaidia msanii kucheza vyombo na kuurekodi wimbo live. Alisema gharama kubwa zaidi inaweza kuwa shilingi milioni moja na gharama ndogo tu za kuwawezesha wapiga vyombo wakati wa kufanya mazoezi.

Kwahiyo inawezekana kabisa kutengeneza wimbo mzuri na uliokamilika kwa gharama ndogo na pindi unapoipa video nzuri, una uhakika wa kuwa na wimbo utakaodumu kwa miaka mingi bila kuchosha masikio ya wapenzi wa muziki. Ni kwasababu kamwe haitakuja kutokea muziki uliotengenezwa na mtu mmoja kuwa sawa na ule uliotayarishwa na watu wengi na tena live.

Kwahiyo inawezekana kabisa kuwa na nyimbo zitakazofanya vizuri bila hata kuwa na video. Video ni muhimu sana kwenye tasnia ya muziki lakini wasanii waache kuweka nguvu nyingi huko na kusahau kutengeneza muziki mzuri.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents