Tigray: Watu 350,000 wanakabiliwa na njaa
Ripoti ya Umoja wa Mataifa na mashirika ya kutoa msaada iliyochapishwa jana Alhamis, inasema watu 350,000 katika jimbo la Tigray nchini Ethiopia wanakabiliwa na baa la njaa na wengine zaidi ya milioni 2 wanakaribia kutumbukia katika janga hilo.
Ripoti hiyo imeongeza kuwa tatizo hilo limechangiwa na mgogoro unaoendelea ambao umewalazimu maelfu ya watu kuyakimbia makaazi yao, upatikanaji hafifu wa misaada ya kiutu, kupoteza mazao na kipato.
Tathmini ya Shirika la kufuatilia viwango vya hali ya usalama wa chakula IPC, imebaini kwamba angalau asilimia 20 ya kaya zinakabiliwa na ukosefu kamili wa chakula, njaa, kifo na umaskini vinashuhudiwa.
Aidha utapiamlo umedhihirika kwa zaidi ya asilimia 30 ya kaya. Tigray ilikumbwa na mapigano tangu mwezi Novemba kati ya wanajeshi wa serikali na vikosi vya mkoa huo.