Uhasibu wagomea ongezeko la ada
Wanafunzi wa Chuo cha Uhasibu cha Jijini Dar es salaam (TIA), jana walifanya mgomo wa kutoingia Madarasani wakiulalamikia uongozi wa Chuo hicho kuwapandishia ada kwa zaidi ya asilimia hamsini, suala ambalo hawajakubaliana nalo.
Wakizungumza Chuoni hapo , baadhi ya viongozi wa Serikali ya wanafunzi akiwepo Makamu wa Rais wao Mbaraka Athumani, walisema wanafunzi hao wamechukizwa na tamko la uongozi wa Chuo la kuwazuia wanafunzi wote watakaoshindwa kulipa ada kufanya mitihani inayotarajiwa kuanza wiki tatu zijazo.
Gari la Polisi likiwa limezuiliwa kuingia katika Chuo cha Uhasibu wakati wa mgomo huo
Alisema kwa kawaida ada halali ya Chuo hicho ambayo bado wanaitambua ni Sh.650,000 kwa wanafunzi wa uhasibu na Sh.600,000 kwa wanafunzi wa ununuzi na ugavi huku wakidai wanachopingana nacho ni ada hiyo kupandishwa kwa mara mbili yake na kufikia Sh.Milioni 1.2 na Sh. Milioni 1.3.
Naye Msemaji wa Serikali ya wanafunzi wa Chuo hicho, Evans Krispin, alisema mbali ya matatizo hayo ya ada pia Chuo hicho kinakabiliwa na kero matatizo mbalimbali ikiwemo ya kutokuwemo kwa Maktaba, Chumba cha Kompyuta na miundombinu mibovu, na kusisitiza kuwa kero hizo ni muda mrefu.