Uturuki na Ufaransa hali si shwari, kibonzo cha Rais Erdogan chachochea
Rais wa Uturuki Rwecep Tayyip Erdogan ametoa hasira yake kuhusu kibonzo alichosema “kinachukiza” cha jarida la tashtiti la Kifaransa linalochapishwa kila wiki la Charlie Hebdo kikimuonesha akiwa ameishika sketi ya mwanamka na kumchungulia makalio huku akinywa bia wakati amevaa nguo za ndani.
Ofisi ya Erdogan imeapa kuchukua “hatua ya kisheria na kidiplomasia” wakati televisheni ya Uturuki ya NTV imesema serikali pia imemuita naibu balozi wa Ufaransa kulaani tukio hilo.
Picha za kumpinga Macron zimekuwa zikichorwa kwenye ukuta wa mji wa Gaza katika Palestina
Ufaransa ilimuita mjini Paris balozi wake wa Uturuki kwa ajili ya mashauriano katika ishara zaidi ya kuzorota mahusiano ya kidiplomasia kati ya washirika hao wawili wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO.
Katuni hiyo ya ukurasa wa mbele wa jarida la Charlie Hebdo ilikuja siku kadhaa baada ya Erdogan kutoa wito wa kususia bidhaa za Ufaransa na kuhoji hali ya kiakili ya Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron kwa kuchochea hisia dhidi ya Uislamu.
Kumeshuhudiwa maandamano ya hasira kote Uturuki na maeneo mengine ya ulimwengu wa Kiislamu kupinga matamshi ya Macron.