Ajali mbaya ya mabasi mawili ya kampuni moja yaua 29 Singida
Ajali mbaya ya gari iliyohusisha mabasi mawili ya kampuni ya City Boys imesababisha vifo vya takriban watu 29 Jumatatu hii.
Ajali hiyo imetokea mchana ambapo moja basi namba T531 BCE likitokea Dar kwenda Kahama na jingine namba T 247 likitoka Kahama kwenda Dar yote ya City Boys yaligongana uso kwa uso.
Abiria mmoja aliyenusurika amedai kuwa ajali hiyo imetokea baada ya madereva wa mabasi hayo kutaka kupeana ishara ya kusalimiana.
“City Boy ya Kahama ilikuwa mbele kutoka Dar na yetu ilikuwa mbele kutoka Kahama kwahiyo huwa ni ishara zao kupongezana kuleteana magari, dereva wa gari yetu hakuwa mzoefu wa hayo mambo kwahiyo mpaka hiyo hali inatokea dereva wangu ilibidi ampishe ndio akatupiga mtama,” amesema.
Ajali hiyo imetokea Maweni nje kidogo na mji wa Manyoni mkoani Singida.
Kamanda wa polisi mkoa Singida Thobias Sedoyeka amedai watu 24 walipoteza maisha hapo hapo. Wengi wamejeruhiwa.
Idadi ya watu waliopoteza maisha inahofiwa kuongezeka. Rais Dkt John Magufuli ametuma salam za rambirambi kwa familia za watu waliopoteza maisha.