Simba SC yatoa siku nne kwa wachezaji wake
Mabingwa wa michuano ya FA klabu ya Simba imetoa mapumziko ya siku nne kwa wachezaji wake kabla ya kukutana tena siku ya Ijumaa ya wiki hii.
“Kikosi cha wekundu wa Msimbazi, Simba Sports Club kinatarajia kuanza mazoezi rasmi ijumaa hii baada ya mapumziko yaliyoanza leo.”
Wakati kikosi cha Simba kikitaraji kukutana tena Desemba mosi, Ligi Kuu Tanzania Bara inatarajiwa kusimama kwa muda ili kupisha michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati (CECAFA Challenge) huku wachezaji wakipata nafasi ya kwenda kujiunga na timu zao za taifa.
Kikosi cha Simba kitakwenda mapumziko huku ikiwa inaongoza katika msimao wa Ligi Kuu kwa kuwa na jumla ya pointi 23 baada ya mchezo wao wa mwisho kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Lipuli FC ya Iringa siku ya Jumapili Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Nafasi ya pili ikishikwa na Azam FC yenye alama 23 ambayo nayo imetoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Mtibwa Sugar Uwanja wa Azam Complex Chamazi na nafasi ya tatu ikishikiliwa na Yanga SC yenye pointi 21 ambayo nayo ikitoka sare katika mchezo wake wa mwisho wa bao 1-1mbele ya Tanzania Prisons huku mpaka sasa timu hizo zikiwa zimecheza jumla ya michezo 11.