Uchaguzi Yanga kufanyika bila kujali kupingwa na wanachama, wanaomtaka Manji washauriwa kumchukulia fomu
Uongozi wa klabu ya Yanga umefikia makubaliano na Shirikisho la soka Tanzania (TFF) juu ya uchaguzi wa klabu hiyo uliopangwa kufanyika January 13, 2019.
Uchaguzi huo wa kujaza nafasi zilizowazi utafanyika kama ulivyopangwa ambapo Yanga na TFF zimekubaliana kuwa Kamati zote mbili za uchaguzi ya TFF na Yanga zitashirikiana kuusimamia uchaguzi huo
Katika tamko lililotolewa na TFF mbele ya waandishi wa habari mapema leo, uchaguzi huo utafanyika bila ya kujali kupingwa na baadhi ya wanachama wa klabu ya Yanga
Aidha, kwa wale ambao wamekuwa wakisisitiza kumtambua Yusufu Manji kama Mwenyekiti wa Yanga, wameshauriwa wamshawishi na hata kwenda kumchukulia fomu ili aweze kugombea tena nafasi hiyo
Uchaguzi huo utahusisha nafasi ya Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na nafasi nne za Wajumbe wa Kamati ya Utendaji
Hata hivyo Thobias Lingalangala ameteuliwa kuwa kaimu mwenyekiti wa klabu hiyo ya Yanga kufuatia kikao kilichofanyika jana ambacho kiliwahusisha viongozi wa pande zote mbili TFF na Yanga na leo kutangaza rasmi mchakato wa uchaguzi wakati ada ya fomu ya kuwania nafasi ya uongozi ni shilingi laki 2 ambazo ni mwenyekiti na makamu huku wajumbe ikiwa ni shilingi laki moja.