Arnold Kayanda ajiunga na BBC Swahili
Habari njema kwa mashabiki wa aliyekuwa mtangazaji wa kituo cha Radio Clouds FM, Arnold Kayanda ni kuwa hivi karibuni ataanza kusikika tena Radioni baada ya kujiunga na Shirika la Utangazaji la BBC Swahili.
Baruan Muhuza, Regina Mwalekwa na Arnold Kayanda
Kayanda ambaye amejipatia umaarufu zaidi kupitia vipindi mbalimbali vya Clouds kikiwemo kipindi cha Top 20 pamoja na Jahazi, ameitoa habari njema kwa wasikilizaji wake kupitia ukurasa wake wa Facebook.
Huu ndio ulikuwa ujumbe wa kwanza alioandika jana:
“Siku yangu ya kwanza katika #BBCSwahili. Miongoni mwa walionipokea ni dada yangu Regina Mwalekwa. Hapa tukiwa na ndugu yetu Baruan Muhuza (kushoto). Picha nikiwa na wanafamilia wengine itafuata hivi punde.” Aliandika chini ya picha aliyopiga na Baruan Muhuza na Regina Mwalekwa.
Na hiki ndicho alichokiandika leo baada ya kupost picha hii (hapo juu):
“Watu hawa (wengine hawapo pichani) walinipokea vizuri hadi nikaogopa pengine wameshanitafutia mteja wanasubiri nilale waniuze. Hii ni familia yangu mpya. Shukrani sana Dada Liz Massinga, John Solombi, Dada Halima Nyanza, Leonard Mubali, Dada Regina Mwalekwa, Hassan Mhelela, Dada Regina Joseph, Ben Mwang’onda, Eric David Nampesya, Baruan Muhuza na wengine wote. Mungu ameshanifikisha nchi ya ahadi kilichobaki ni kumtumikia. Sasa vijana waambie vijana wenzenu nao wawaambie wenzao katika ratiba zao watenge muda wa kuisikiliza Idhaa ya Kiswahili ya #BBC.”
Kayanda ameungana na Regina Mwalekwa ambaye pia amejiunga na kituo hicho cha kimataifa hivi karibuni akitokea Clouds FM.