Bila kazi ya ziada ukitegemea muziki unaweza kuumbuka town – Stereo
Rapper Stereo amedai kuwa muziki wa Tanzania ni mgumu kiasi kwamba kama msanii hana shughuli zingine za kujiingizia kipato anaweza kuumbuka.
Stereo ameambia Bongo5 kuwa licha ya kutangaza kujikita zaidi kwenye kufanya muziki baada ya kumaliza masomo yake, amegundua kuwa muziki hauwezi kuwa tegemeo la wasanii.
“Ni kweli nimeongeza muda wangu zaidi kwenye muziki, ambao nilikuwa naukosa kutokana na chuo, lakini pia imenibidi nifanye shughuli nyingine za kujiongezeA kipato kwa sababu muziki sio all way the business, siO all way the kind of business una msimu wake,” amesema.
“Kwa mfano msimu kama huu hakuna show, kwahiyo usipokuwa na shughuli nyingine za ziada unaweza ukaaibika. Kwahiyo ninachosema kweli muda nimeuongeza katika shughuli za muziki pia nimeongeza katika shughuli zangu na ujasiriamali,” ameongeza rapper huyo.
Kwa upande mwingine Stereo ameitaka serikali pamoja na wadau mbalimbali kuboresha sheria ya haki miliki ili kuwasaidia wasanii kupata kile wanachostahili.
“Kimsingi haki miliki, tutakapopewa sheria tutapata meno ya kuuma. Tutaweza kulinda kazi zetu na kile ambacho tunakifanya, tutaweza kunufaika. Sasa hivi huwezi ukamzuia mtu ku-download nyimbo zako wakati hakuna sheria, huwezi ukazuia matumizi ya jina lako kwa sababu kuna watu sasa hivi unakuta wanatumia jina lako wewe kwa matakwa yao. So katika hali kama hiyo tukipewa haki tunaweza kusimamia kazi zetu na tutaanza kuona manufaa.”
Wakati huo huo Stereo amedai kuwa video ya wimbo wake ‘Ukonga na Ilala’ aliomshirikisha Chidi Benz itatoka hivi karibuni.