Roma adai tangazo kuwa wimbo wake umefungiwa inamwathiri kiuchumi, aiandikia barua BASATA
Roma amedai kuwa taarifa zilizotolewa kuwa wimbo wake Viva Roma umefungiwa, zimemuathiri kiuchumi.
Akiongea kwenye kipindi cha Planet Bongo cha EA Radio hivi karibuni, Roma alidai kuwa hiyo ndio sababu iliyomfanya atumie wanasheria kuiandikia barua BASATA ili imweleze sababu za kuufungia wimbo wake.
Bado BASATA haijaijibu barua yake.
“Ni kweli hizi taarifa zilikuwa zinaathiri career yangu,” alisema Roma. “Kila mtu aliipokea hiyo taarifa tofauti. Wengine walijua Roma amefungiwa kabisa kwahiyo kuna deal za hapa na pale tukawa tunazikosa, mtu anahisi akimwalika hata Roma kwenye kimeo chake inaweza ikawa ni balaa kumbe sio kweli. Kwahiyo ilikuwa inaniathiri mimi kama kijana wa Kitanzania au kama mzalendo wa nchi yangu ambaye nategemea ugali wangu kupitia hii sanaa, kupitia ajira yangu ya muziki wa hip hop,” alisisitiza.
Hata hivyo pamoja na kuipa BASATA siku tatu ili iweze kujibu barua hiyo bado hajapata majibu na hivyo amepanga kuita waandishi wa habari.
Kwa upande wake katibu mtendaji wa baraza hilo, Godfrey Mngereza alikiri kupokea barua kwa Roma lakini alidai ‘amri’ ya Roma ya kuwataka wajibu barua ndani ya siku tatu haipo kwenye sheria yoyote na wamemruhusu achukue hatua yoyote anayohisi itafaa.