Uncategorized

Facebook yatumika kuwasaka majambazi na kuwaua Nairobi, Mkurugenzi wa upelelezi atokwa na machozi baada ya kusikia ushuhuda

Kundi linaloshukiwa kutekeleza mauaji ya watu ndani ya kikosi cha polisi nchini Kenya kinatumia Facebook kuwalenga na kuwaua vijana wanaoaminika kuwa wafuasi wa magengi ya majambazi, wakaazi wa kitongoji duni katika mji mkuu wa Nairobi wameuambia mkutano wa hadhara.

Kwa mujibu wa shirika la habari la BBC, “Nimepoteza waume zangu wawili katika kipindi cha mwaka mmoja,” mwanamke aliyebubujikwa na machozi huku akimbeba mwanawe ubavuni amewaambia watu waliokusanyika katika holi ya mkutano huko Kayole mjini Nairobi mwezi uliopita.

Wengine walifika mbele na kuhadithia visa kama hivyo kuhusu namna walivyowapoteza wapendwa wao walio na umri wa kati ya miaka 15 na 24.

Mwendesha mashtaka, maafisa wakuu wa polisi, wanaharakati wa kutetea haki za binaadamu ambao pia walikuwa katika mkutano huo, walisikiza kwa makini wakati viongozi wa kijamii walivyoeleza namna vijana hao wanaoshukiwa kuwa wahalifu, walivyolengwa katika makundi tofauti ya Facebook na makundi ya “wawindaji majambazi”.

This image has an empty alt attribute; its file name is wwww.jpg

“Wanawalenga katika Facebook, baada ya wiki moja au mwezi wanawapiga risasi na kuweka picha zao katika Facebook,” Wilfred Olal kutoka kundi la Dandora Community Justice Centre aliuambia mkutano huo.

Picha zinazobandikwa, mara nyingine zikiwa zinaonyesha ukaribu wa vichwa vilivyopasuka na miili iliyochanika, kwa kawaida huchapishwa kwa kutolewa onyo kwamba hatma kama hiyo inawasubiri wahalifu wengine. Baadhi ya picha huzibwa na kampuni ya Facebook lakini mtumiaji mtandao huo ana nafasi ya kuzizibua picha hizo.

Wakaazi hao wa Kayole wanasema kuna makundi tofauti ya Facebook baadhi ya umma na mingine yasio wazi, ambayo picha hizo za kuogofya huchapishwa kila siku.

Machozi ya Polisi

Duncan Omanga, mtafiti katika chuo kikuu cha Moi nchini Kenya, ambaye amekuwa akiyafuatilia makundi hayo katika Facebook kwa miaka mitatu, anasema maafisa wanaoshukiwa wa polisi hutumia majina bandia ya kidijitali kuwafuatilia watu wanaowalenga.

“Ukurasa wa kwanza rasmi wa polisi katika Facebook ulionekana chini ya jina la Hessy wa Kayole.

“Hessy aligeuka kuwa muindaji wahalifu anayesikika tu, lakini hajulikani ni nani.”

Huku taarifa kumhusu zikienea katika mitandao ya kijamii, akaunti zaidi zenye majina ya wawindaji wahalifu kutoka maeneo mengine yanayokabiliwa na visa vya uhalifu zikaanza kuchomoza.

Kwa mujibu wa Bwana Omanga, ilionekana kuwa ni hatua ya makusudi kutoa taswira ya “kusambaa kwa polisi na ujasusi wa ‘serikali’ ” katika maeneo hayo ya Nairobi.

Mnamo Novemba mwaka jana, aliyekuwa mkuu wa polisi Joseph Boinnet alisema, “Mtu aliyefungua akaunti hizo za Facebook sio afisa wa polisi, lakini [ni raia] aliye na shauku kuhusu masuala ya usalama.”

Na mkurugenzi wa upelelezi (DCI), George Kinoti, aliyebubujikwa na machozi wakati akisikiza baadhi ya ushuhuda uliotolewa huko Kayole, aliuambia mkutano huo kwamba hawafahamu maajenti kama Hessy.


“Ninasema hakuna atakayemfichia afisa wa polisi anayetekeleza mauaji chini ya uangalizi wangu.”

Lakini kauli yake ilimezwa kwa kelele za umati, huku mtu mmoja akipiga kelele, “Wako kwenye Facebook, na pia Twitter.”

Mkutano huo huko Kayole uliandaliwa na mkurugenzi wa mashtaka ya umma (DPP) baada ya wanaharakati na wakaazi kusema kwamba polisi hawatilia maanani kilio chao.

Kukutana na Mungu

Utafiti wa Omanga umeashiria kwamba katika mwezi mmoja, washukiwa sita wa ujambazi wanalengwa , taarifa kuhusu tuhuma za uhalifu wao na maeneo wanayohudumu na aina ya silaha wanazoaminika kutumia huchapishwa katika akaunti na makundi tofuati kwenye Facebook.

Katika kipindi hicho, kati ya visa 10 hadi 12 vya mauaji yaliotekelezwa na polisi – ya washukiwa wa ujambazi huchapishwa katika kundi lisilo wazi katika Facebook liitwalo Nairobi Crime Free.

Ni kundi lenye wafuasi 300,000 na lenye ujumbe: “Ni Mungu tu anayewasamehe magaidi, lakini kuwakutanisha na Mungu ni jukumu letu”, ikiambatana na picha ya mwanamume huyo asiyejulikana akiwa amevalia magwanda na kofia ya kijeshi.

Facebook/ Nairobi Crime Free

Omanga anasema picha hizo zinazosambazwa katika kundi hilo zimenuiwa kushtusha na kuonyesha ujasiri. Mara nyingine picha ya zamani ya muathiriwa huwekwa kando ya picha ya mwili wake baada ya kuuawa .

Wafuasi wa kundi hilo wanaonekana kufurahishwa na yanayosambazwa katika kundi hilo kwa kuangalia namna wanavyopenda na kuonyesha ishara za kufurahia yaliomo katika sehemu ya maoni yanayoachwa katika kila ujumbe unaochapishwa.

Baadhi huelezea wanayoyapitia binafsi kama waathirika wa uhalifu na kutoa wito kwa polisi kuwaangamiza wahalifu wengine.

Ili kuruhusiwa kuwa mfuasi wa makundi hayo, ni lazima mtu ajibu maswali matatu likiwemo iwapo wanaunga mkono jitihada za polisi kupambana na uhalifu.

Wahalifu pia hufuatilia kwa makini makundi hayo kwenye Facebook kutegea kujuwa iwapo wao ni miongoni mwa walioorodheshwa kulengwa na kuangamizwa.

Vijana wengi wameishia kujificha baada ya kulengwa au wamelazimika kutafuta ulinzi kutoka mashirika ya kutetea haki za binaadamu.

Omanga anasema polisi walipata pia kujua kuhusu makundi ya magengi kupitia kurasa za Facebook wakati wafuasi walipotumia akaunti zao binafai kujionyesha na pia kuwatishia maafisa.

‘Gengi la Gaza laangamizwa

Lakini hili limesita pakubwa tangu mkuu wa gengi, Mwani Sparta, anayefahamika kwa kuchapisha picha kuhusu maisha yake ya uhalifu, alipoiweka picha yake mnamo 2017 akiwa ameshikilia bunduki ya rashasha akiwa na wenzake.

R: Mwani Sparta, a known gangster in Kenya, who it is suspected was targeted in an extrajudicial killing L: Mwani Sparta, the checked shirt, with members of his gang

Alitambua makosa yake na akaitoa picha hiyo – lakini tayari ilikuwa imesambazwa na polisi walipata kufahamu mengi kuhusu waliomo katika gengi hilo la Gaza.

Wote wakawa washukiwa mauaji ya kiholela. Kila wakati mfuasi wa kundi la Gaza alipouawa, picha hiyo ilichapishwa katika Facebook huku nyuso za waliouawa zikitiwa alama, Omanga amesema.

Mfuasi mwingine wa gengi hilo , ambaye picha yake pia ilisambazwa, alionekana kuwa na uoga mwingi na mauaji hayo kiasi cha kuchapisha katika Facebook ujumbe kwamba amejitoa katika maisha ya uhalifu na kwamba ameokoka katika dini ya kikristu – na alikamatwa baada ya hapo.

Lakini sio wahalifu wanaolengwa katika makundi hayo ya Facebook . Wanaharakati wa kutetea haki za binaadamu wanasema kwamba hata wao wamo katika tishio kwa kuzungumzia kuhusu mauaji hayo ya kiholela.

“Tunataka kujua iwapo watu hawa kama Hessy, ni maafisa wa polisi, na iwapo ni polisi, je wana haki ya kuwaua watu na kubandika picha za miili yao katika Facebook?”

Picha za kuogofya marufuku

Kundi moja linalojiita Uhai Wetu, sasa limeundwa ili wanaharakati wa haki za binaadamu kutoka vitongoji tofuati waweza kusaidiana katika kutoa muitikio dhidi ya matishio kama hayo.

Wameiomba Facebook mara kwa mara izitoe picha hizo za kudhalilisha, ambazo wanasema zinakwenda kinyume na viwango vya maadii ya jamii, lakini licha ya jitihada kadhaa hawajafanikiwa, mtafiti mmoja kutoka kundi hilo ameiambia BBC.

Msemaji wa Facebook ameeleza kwamba mtandao huo una sheria za wazi dhidi ya kuchapisha picha za kuogofya na uhalifu na “wakati tunapoarifiwa kuhusu picha hizo tunaziondoa”.

“Uchunguzi wetu katika suala hili unaendelea na tunaishukuru BBC kwa kuliangazia ,” Facebook imeongeza.

Hatahivyo, hakujakuwa na kilio cha jumla kuhusu mauaji haya, isipokuwa kutoka kwa jamii inayoathirika.

Wilfred Olal hands over print outs to the state prosecutor Noordin Haji (l)

Mwanaharakati Wilfred Olal (kulia) akabidhi baadhiya chapisho katia akaunti ya Hessy kwa mkurugenzi mkuu wa mashtaka ya umma mwezi uliopita

Omanga anasema afisa wa polisi asiyetaka upuuzi na ambaye ana shauku kubwa, ame pokea ombi la Wakenya wengi waliochoshwa na wanachokiona kuwa ni mfumo wa sheria uliokumbwa na usfisadi na unaochukua muda.

Taarifa katika vyombo vya habari Kenya miaka michache iliyopita kuhusu “super cops” au polisi jasiri Nairobi imetoa “kibali cha kutekeleza mauaji”, mtafiti huyo anasema.

Kwa Bwana Olal, anayekiri kwamba uhalifu ni tatizo kubwa katika baadhi ya maeneo Nairobi, anaeleza kwamba ni suala la sheria kutekelezwa kwa usawa.

“Iwapo washukiwa wa wizi wa kodi nchini walio matajiri wanapelekwa mahakamani, basi pia tunataka vijana wetu washtakiwe kwa haki,” anasema.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents