Kiongozi wa kundi la kigaidi la Al-Qaeda, Ayman al-Zawahiri aja na mbinu mpya ya kuishambulia Marekani
Kiongozi wa kundi la kigaidi la Al-Qaeda, Ayman al-Zawahiri amewataka Waislamu duniani kote waungane na kutangaza vita dhidi ya Marekani kwani taifa hilo ndio adui mkubwa wa Uislamu duniani.
Kupitia video iliyorekodiwa kwa dakika 30 na kutolewa na kundi hilo mtandaoni, inamuonesha Ayman al-Zawahiri akimshutumu Rais wa Marekani, Donald Trump kuwa ndiye mtu hatari zaidi katika kuudhoofisha uislamu mashariki ya kati.
Amesema Marekani imeisaidia Israel kuchukua mji wa Yerusalemu ambao yeye amedai kuwa ni mji halali wa Palestina, hatua ambayo imesababisha Wapalestina wengi ambao ni Waislamu kuteseka na kuuawa na Wayahudi.
“Marekani imekuwa adui mkubwa wa kwanza wa Uislamu, ingawaje nchi hiyo serikali yake haifungamani na dini yoyote lakini sera nyingi zinaonekana kuiangamiza dini yetu, nawaomba Waislamu duniani kote tuungane“amekaririwa Ayman al-Zawahiri akiongea kwenye video hiyo.
Ayman al-Zawahiri amewataka Waislamu kwa kila nafasi watakayoipata kutekeleza mashambulizi ya kigaidi ili kulinda hadhi ya Uislamu duniani.
Kauli ya Ayman al-Zawahiri imetoka wiki hii ambayo Marekani inaadhimisha miaka 17 tangu shambulizi la kigaidi la Septemba 11 la mwaka 2001 litekelezwe na kundi hilo la kigaidi.
Jana Rais wa Marekani, Donald Trump akihutubia maelfu ya watu katika kuadhimisha siku hiyo, alisema kuwa taifa lake halitamruhusu gaidi yoyote kufanya shambulizi nchini mwake na yupo tayari kwa gharama yoyote.
Tukio la Septemba 11 ndio tukio la kigaidi kubwa zaidi kuwahi kutokea Marekani, na imakadiriwa zaidi ya watu 3,000 walipoteza maisha kwenye shambulizi hilo.