Sanaa Kutumika Kuboresha Maisha
Wanajamii wametakiwa kutumia kazi za sanaa za mikono za wasanii wa hapa nchini katika kupamba nyumba zao ili kuongeza hamasa na maendeleo ya tasnia hiyo hapa nchini. Wito huo ulitolewa juzi na Mdau wa sanaa za uchoraji Candida Bahame ambae ni Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Nyayo Za Mama wakati akizindua maoenesho ya wiki mbili ya kazi zake za sanaa.
Candida alisema kuwa wasanii wa hapa nchini wanao uwezo wa kuchora na kutengeneza picha kwa kutumia viashiria mbalimbali vya kisanii ambavyo zinapendezesha nyumba.
Alisema kuwa wanajamii wakiwa na utamaduni wa kununua kazi zao za sanaa na kuzipamba majumbani kwao watakuwa kwa kiasi kikubwa wamesaidia kukua kwa sanaakiwa kama mdau wa kazi za sanaa ya uchoraji hapa nchini.
“Mimi naona kuwa muda umefika kwa hoteli zetu, ofisi na hata nyumba zetu watu kutumia picha za wasanii wa hapa nchini katika kupamba nyumba zao ili kuonesha kuwa wanathamini na kutambua sanaa zetu hapa nchini” alisema Candida.
Akizungumzia sanaa yake hiyo ambayo alisema kuwa alianza tangia miaka ya 1980, Candida alisema kuwa gharama ya picha zake anazipanga kulingana na muda aliotumia kuzichora pamoja na umaridadi wa picha hizo.
Alisema kuwa anatumia kipaji chake kufikisha ujumbe kwa njia ya maneno ambapo anatumia shanga kushona maneno yenye ujumbe na pia anatumia shanga kutengenezea picha.Maonesho hayo ya wiki mbili yanaendelea katika Ujamaa Art Gallery