HabariSiasa

Saratani ya Mfalme Charles wa III sio ya Tezi dume ila ana uvimbe kwenye tezi dume

Mfalme Charles wa Uingereza amegunduliwa kuwa na saratani, Kasri la Buckingham limetangaza.

Saratani hiyo si ya tezi dume, lakini imegunduliwa hivi karibuni wakati akipatiwa matibabu ya uvimbe katika tezi dume.

Kasri la Buckingham hata hivyo halijaweka wazi aina ya saratani ambayo Mfalme Charles aliyogunduliwa kuwa nayo, lakini kwa mujibu wa taarifa kutoka kwenye kasri hilo, tayari Mfalme ameanza “matibabu ya kawaida leo Jumatatu.

Kasri la Buckingham linasema kwamba Mfalme “anasalia na mtazamo chanya juu ya matibabu yake na anatazamia kurejea kutekeleza kazi kamili ya umma haraka iwezekanavyo”.

Ataahirisha shughuli zake za umma na inatarajiwa kwamba wanafamilia wengine wakuu wa familia ya kifalme watamsaidia shughuli zake za umma wakati wa matibabu yake.

Hakuna maelezo zaidi yaliyotolewa juu ya hatua ya saratani au matibabu atakayopewa.

Ingawa atasitisha hafla zake za umma, Mfalme, mwenye umri wa miaka 75, ataendelea na jukumu lake la kikatiba kama mkuu wa nchi.

Alionekana kwenye ibada ya kanisa huko Sandringham siku ya Jumapili, ambapo alipungia mkono umati.

Alifanyiwa upasuaji wa tezi dume katika hospitali ya kibinafsi ya London zaidi ya wiki moja iliyopita.

Mfalme alikuwa amechagua kujitokeza hadharani kuhusu matibabu yake ya tezi dume, kwa lengo la kuwahimiza wanaume zaidi kupata uchunguzi wa kibofu, ilisema kasri wakati huo.

Alisemekana kuwa alifurahishwa na kuongeza ufahamu kuhusu suala hilo, na tovuti ya NHS ikiripoti kuongezeka kwa masuala kuhusu hali ya tezi dume.

Kwa aina nyingi za saratani, nafasi ya kuipata huongezeka kadri umri unavyoongezeka. Takwimu za Uingereza zinaonyesha, kwa wastani kila mwaka, zaidi ya theluthi (36%) ya kesi mpya za saratani zilikuwa kwa watu wenye umri wa miaka 75 na zaidi.

Waziri Mkuu Rishi Sunak amemtakia Mfalme “afueni kamili na ya haraka”, kiongozi wa chama Kikuu cha upinzani cha Labour Sir Keir Starmer pia amemtakia kheri Mfalme.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents