Habari

Serikali yachukua hatua kuhakikisha hali ya chakula na lishe ni imara nchini

Serikali chini ya wizara ya kilimo imesema imeshachukua hatua za kuhakikisha kuwa hali ya chakula na lishe ni imara nchini.

Hayo yamesemwa Jumanne hii na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Dkt. Charles Tizeba mjini Dodoma katika Kikao cha sita cha bunge alipokuwa akitoa kauli ya Serikali kuhusu hali ya chakula na lishe kwa mwaka 2016/2017.

Dkt Tizeba alisema, “Tathimini imebainisha kuwa halmashauri za wilaya 55 zinahitaji jumla ya tani 1,969 za mbegu bora za mahindi, mtama na mizizi inayokomaa kwa muda mfupi na kustahimili ukame. Mbegu hizo zinahitajika ziwafikie mwezi Februari 2017 iliziweze kupandwa katika msimu wa 2016/2017 katika maeneo yanayoendelea kupata mvua wakati huu wa mwaka.

Tizeba alizitaja hatua ambazo serikali inazichukua kuhakikisha kuwa hali ya chakula na lishe ni imara kuwa ni pamoja na kusimamia usambazaji wa mbegu za mazao ya kilimo zinazostahimili ukame na zinazozaa kwa muda mfupi ambazo ni pamoja na mtama, uwele na mbegu za mazao aina ya mizizi za mihogo na viazi vitamu ili kuzitumia vizuri mvua zinazonyesha sasa.

Aidha amesema kuwa kutokana na hali ya mwenendo wa unyeshaji wa mvua za vuli na msimu kutoridhisha katika maeneo mengi ya nchi, wakuu wa mikoa na wilaya wanashauriwa kuendelea kuhamasisha na kusimamia wakulima kutuma mbegu zinazokomaa mapema na kupanda mazao yanayostahimili ukame.

Sambamba na kuzungumza hayo wizara hiyo imewataka wakulima kuendelea kuzitumia mvua zinazoendelea kunyesha kwa kupanda mazao yanayostahimili ukame na kukomaa kwa muda mfupi na pia waendelee kutunza na kutumia chakula walichonacho kwa uangalifu.

BY: Emmy Mwaipopo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents