Wabunge leo kumuaga marehemu Sitta
Mwili wa aliyekuwa Spika wa Bunge la 9 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samuel Sitta unatarajiwa kuagwa leo mchana na wabunge wa Bunge hilo katika viwanja vya Bunge vya mjini Dodoma.
Kauli hiyo imetolewa na Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai, alipokuwa akitoa ratiba ya kuuaga mwili wa spika mstaafu itakayoanza mara baada ya kumalizika kwa shughuli za Bunge za kipindi cha asubuhi.
Aidha Mhe. Ndugai amesema kuwa Bunge linatarajia kuupokea mwili wa mpendwa huyo leo mnamo majira ya saa 8 mchana kutoka katika uwanja wa ndege wa Dodoma na kupelekwa moja kwa moja ndani ya Bunge hilo kwa ajili ya kupewa heshima za mwisho na wabunge.
“Baada ya mwili wa mpendwa wetu kuwasili katika viwanja hivi, tutakuwa na kikao maalum cha Bunge kitakachofanyika mida ya saa 8:30 mchana ambapo wabunge watapata nafasi ya kutoa salamu za rambirambi na baadaye utaratibu wa kutoa heshima za mwisho utafuata”, alisema Mhe. Ndugai.
Awali mwili wa marehemu Sitta unaagwa kwenye viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.
BY: EMMY MWAIPOPO