Ole Gunner Solskjaer kutupa karata yake ya kwanza Old Trafford, mashabiki wamuandalia mabango ’20LEGEND’
Mashabiki wa klabu ya Manchester United hii leo wanahamu kubwa ya kumshuhudia kocha wao mpya, Ole Gunner Solskjaer akishuka kwenye uwanja wa nyumbani wa Old Trafford kwa mara ya kwanza toka kukabiziwa timu hiyo ambapo atawakabili Huddersfield.
Mashetani hao wekundu wakiwa chini ya Solskjaer walipata ushindi wa jumla ya mabao 5 – 1 dhidi ya Cardiff City kwenye mchezo wake wa kwanza siku ya Jumamosi iliyopita.
Hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza kwa United kufunga mabao mengi kwenye mchezo mmoja tangu mara ya mwisho ilipowahi kufanya hivyo chini ya kocha Sir Alex Ferguson ambapo walitoka sare ya 5-5 dhidi ya West Brom mwezi Mei mwaka 2013.
Kwenye mchezo wao huko Wales, mashabiki wa United walitoa heshima zao kwa Solskjaer kupitia mabango yaliyoandikwa ’20LEGEND’ ambapo siyo aina mpya ya mabango bali yaliwahi kutumika kipindi hicho wakati kocha huyo akiwa mchezaji akivalia jezi namba 20 kabla ya kustaafu.